27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SIASA ZIWEKWE KANDO DENI LA UMEME

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema iwapo Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) litaikatia umeme Zanzibar kutokana na deni wanalodaiwa, wataweza kurudi katika matumizi ya asili ambayo ni kutumia vibatari kupata mwanga.

Kauli hiyo ya Dk. Shein  ambayo aliisema mara baada ya kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Aman Abeid Karume, akitokea nchini Indonesia katika mkutano maalumu aliomwakilisha Rais Dk. John Magufuli imekuja baada ya Tanesco kutoa siku 14 kwa wadaiwa sugu kulipa deni kabla ya kukatiwa umeme .

Alhamisi wiki hii Tanesco ilitoa siku 14 kwa wadaiwa wote sugu, ikiwa ni pamoja na Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco), linalodaiwa Sh bilioni 127, kulipa deni hilo ndani ya muda huo kabla ya kukatiwa umeme.

Wiki iliyopita, Rais Dk. Magufuli aliiagiza Tanesco kukata umeme kwa wadaiwa wote sugu, akisema hata kama Ikulu ya Magogoni inadaiwa, nayo pia ikatiwe nishati hiyo.

Juzi mara baada ya Dk. Shein kuwasili, alizungumzia mafanikio ya safari yake ikiwa ni pamoja na mipango ya viwanda, kauli iliyofanya waandishi kuuliza viwanda hivyo vitaendeshwa vipi ilhali Tanesco imetangaza kuikatia umeme Zanzibar.

Kutokana na swali hilo alisema anaamini Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Serikali ya kiungwana, inayojali watu wake, hivyo haiwezi kufanya hivyo kwenye suala hili la kuzima umeme visiwani Zanzibar na iwapo ikitokea umezimwa, Zanzibar watakuwa tayari kurudi kwenye matumizi ya vibatari.

Kwamba alipokuwa safarini alisoma magazeti mawili yaliyoandika juu ya Zanzibar kukatiwa umeme, lakini haamini kama taarifa hizo zina ukweli, huenda waandishi walinukuu vibaya vyanzo vya taarifa hiyo.

Kwa mujibu wa Dk Shein kwa kipindi cha miaka mingi, ikiwa ni pamoja na wakati yeye akiwa Makamu wa Rais wa Tanzania, Zanzibar imekuwa ikidaiwa na Tanesco na wamekuwa wakilipa kwa utaratibu maalumu, hivyo ni utaratibu maalumu huo ambao unapaswa kutumika ili kuondoa hali hiyo.

Kaimu Mtendaji wa Tanesco, Dk. Tito Mwinuka, amekaririwa na vyombo vya habari wiki hii akisema hadi sasa shirika hilo linadai zaidi ya Sh. bilioni 275 kwa Zeco, wizara, taasisi za Serikali na makampuni ya watu binafsi.

Kwamba jambo hilo limechangia kurudisha nyuma utendaji wa shirika hilo katika kusambaza huduma ya umeme nchini.

Kwa mujibu wa Mwinuka, baada ya muda waliotoa kwisha bila deni hilo kulipwa, Tanesco itachukua uamuzi mgumu wa kuwakatia umeme wadaiwa hao.

Katika deni hilo, Zeco inadaiwa Sh bilioni 127, mashirika ya serikali, wizara na taasisi Sh bilioni 52, huku kampuni binafsi na wateja wadogo wakidaiwa Sh bilioni 94.

Tunasema malimbikizo hayo yamekuwa yakikwamisha jitihada za utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya msingi ndani ya shirika hilo.

Tunaamini Tanesco inahitaji fedha kwa uendeshaji wa shughuli mbalimbali, ikiwamo matengenezo ya miundombinu na utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwamo usambazaji umeme ili huduma hiyo iwafikie watu wengi zaidi.

Tunadhani ulipaji wa bili za umeme hauhitaji siasa. Si sahihi kwa Zanzibar kusema kuwa kwa kipindi cha miaka mingi Zanzibar imekuwa ikidaiwa na Tanesco na wamekuwa wakilipa kwa utaratibu maalumu.

Tunatoa rai kuwa utaratibu huo maalumu umalize deni na bili ziwe zinalipwa kwa wakati kama inavyofanyika kwa malipo mengine na kwa wengine.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles