NEW DELHI, INDIA
WAISLAMU wa dhehebu la Shia nchini India, Anjuman-e-Haideri wamesema watalipia gharama za matibabu yote ya Ibraheem Zakzaky, ambaye ni kiongozi wa kundi la Shia lililopigwa marufuku nchini Nigeria.
Sheikh Zakzaky na mke wake, ambao wamekuwa gerezani kwa miaka minne sasa nchini Nigeria, waliwasili nchini India Jumatatu wakisindikizwa na walinzi wa serikali kuhakikisha wanarudi baada ya kupewa ruhusa ya kwenda kutibiwa nchini humo.
Katibu Mkuu wa Anjuman-e-Haideri, Bahadur Naqvi, aliliambia Shirika la Utangazaji la Uingereza la BBC kuwa wameiandikia barua hospitali ya Medanta ambako Sheikh Zakzaky na mkewe wamelazwa kuhusu kuwalipia gharama zote za matibabu.
“Tuna ripoti ya kitabibu na itawachukua miezi sita kutibiwa, na madaktari wanasema inaweza kuchukua mwaka mmoja au miwili kwa sababu ya sumu iliyoko kwenye damu yake,” alisema Naqvi.
kwa msingi wa ripoti waliyopatiwa na hospitali hiyo alisema kuwa wanakadiria gharama za matibabu kuwa Dola za Marekani 500,000 (£414,000).
Hata hivyo hakusema iwapo hospitali ya Gurgaon imekubali msaada huo.
Anjuman-e-Haideri si kundi pekee linalotaka kusaidia gharama za matibabu ya Sheikh huyo.
Tume ya Kiislamu ya Haki za binadamu ya nchini Uingereza (IHRC) pia imeripotiwa kutaka kusaidia matibabu yake, lakini chanzo cha habari kililidokeza BBC, kuwa huenda mamlaka za nchini India isiipe nafasi hiyo kwa kuwa ni taasisi ya kigeni.
Sheikh Zakzaky (66), anakabiliwa na tuhuma za mauaji na makosa mengine ambayo yote ameyakana.
Pia amekana kwamba taasisi ya Shia aliyokuwa akiingoza ambayo inaendesha hospitali na shule katika baadhi ya majimbo nchini Nigeria eneo la kaskazini inapata msaada kutoka Iran.
Hivi karibuni Serikali ya Nigeria ilitangaza kulifuta dhehebu la Shia kwa kile ilichoeleza kuwa limekuwa sehemu ya machafuko na mipango na kutaka kupora madaraka kupitia huduma inazozitoa kama shule na hospitali.