Na MWANDISHI WETU-DODOMA
NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Antony Mavunde ameeleza jinsi Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ilivyofanikikisha uzalishaji kiwanda cha kutengeneza madawa ya mifugo cha Farm Access kwa kutoa Sh bilioni 1.8.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitembelea maonyesho ya Nanenane katika viwanja vya Nzuguni jijini hapa jana, Mavunde alipongeza juhudi zinazofanywa na benki hiyo na hasa kufanikisha maendeleo ya sekta ya viwanda ikiwemo kiwanda cha Farm Access kilichopo mkoani Dodoma.
“Naomba nichukue nafasi hii kuipongeza TADB na uongozi wake kwa hatua stahiki na madhubuti kuunga mkono azma ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais Dk. John Magufuli za kujenga uchumi wa viwanda hapa nchini,” alisema Mavunde.
Alisema benki ilitoa fedha kwa ujenzi wa kiwanda hadi uzalishaji wake kuhakikisha utengenezaji na upatikanaji wa kutosha wa madawa ya mifugo kiwandani hapo pamoja na kutoa ajira kwa vijana wa kitanzania.
Mbali ya kuvutiwa na bidhaa za kiwanda hicho, Mavunde alimhakikishia Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo wa Kiwanda, Dk. Simon Mphuru kuwa Serikali imejipanga kujenga uchumi unaotegemea viwanda ifikapo mwaka 2025 na kuahidi kukitembelea kiwanda hicho siku chache zijazo.