24.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yataka halmashauri zitoe asilimia ya mapato kwa walemavu

Na RAMADHAN HASSAN-DODOMA


SERIKALI imezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha zinatoa asilimia mbili ya mapato ya ndani kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

Pia, imewataka maofisa maendeleo ya jamii kulielimisha kundi hilo kuhusiana na mikopo inayotolewa na halmashauri ili iwanufaishe.

Agizo hilo lilitolewa jijini hapa jana na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Stellah Ikupa, alipozungumza kwenye wiki ya Asasi za Kiraia (AZAKI).

“Kundi hilo ni miongoni mwa makundi ambayo yanapaswa kupewa elimu lakini pia kuhimizwa  waweze kujiunga katika makundi na hatimaye kuitumia fursa hiyo vizuri na kujiinua katika uchumi,”alisema.

Ikupa aliwataka watu wenye ulemavu kuangalia fursa zinazopatikana katika maeneo yao ikiwa ni pamoja na  kuhakikisha wanakuwa mabalozi wazuri wa kurejesha mikopo hiyo.

“Hakuna haja ya watu wenye ulemavu kuendelea kuwa wanyonge kwa sababu  Serikali imekwisha kuwakomboa kwa kuwapa  mikopo hiyo ambayo pia itawafanya na wao kutegemewa na watu wengine,”alisema.

Akizungumzia ajira kwa watu wenye ulemavu, Ikupa alisema kwa sasa anatembea ofisi kwa ofisi kuangalia kama suala la hilo linazingatiwa kwa kundi hilo.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu  Tanzania (Shivyawata), Ummy Ndelenanga, alisema bado kundi hilo linakabiliwa na changamoto mbalimbali.

Alitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na sekta ya ajira, urasimu wa kupata asilimia mbili ya mapato ya ndani ya halmashauri jambo linalowafanya kushindwa kujikwamua katika uchumi.

Alizitaja changamoto nyingine kuwa ni miundombinu ya usafiri hususan kwenye mabasi ya mikoani, maeneo ya starehe, nyumba za ibada na hoteli bado haijawa rafiki kwa kundi  hilo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles