Na AVELINE KITOMARY-DAR ES SALAAM
NAIBU Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile amesema bado nchi haijafikia hatua ya kusimamisha shughuli za kidini kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID 19) inayosababishwa na virusi vya Corona
Dk. Ndugulile aliyasema hayo jana katika mahojiano yake na MTANZANIA Jumapili.
Alisema a Wizara ya Afya imewashirikisha viongozi wa kidini ili kuhakikisha uwepo wa tahadhari katika nyumba za ibada.
“Tumetoa maelekezo katika sehemu za ibada kwamba viongozi wa kidini wahakikishe wanachukua tahadhari kwa ajili ya mlipuko wa virusi hivi, tumewaelekeza kama mtu ana dalili za mafua asiende kabisa na pia watu wasikusanyane kwa wingi.
“Idadi ya watu iwe ndogo na hata wanapokaa kwenye nyumba za ibada wapishane kwa ‘distance’ (umbali) wasikaribiane hivyo ni jukumu la viongozi na waumini kuchukua tahadhari ili kila mtu ajikinge kwasababu hatutaki kufikia hatua mbaya,”alieleza Dk. Ndugulile.
SOKONI
Aidha kwa upande wa mikusanyiko ya kibiashara alisema Wizara imetoa maelekezo kwa wafanyabiashara wote walioko masokoni kuhakikisha wanatengeneza mazingira ya usafi kwa kunawa mikono kwa maji yanayotiririka na sabuni.
“Kila mmoja, mnunuzi na muuzaji watengeneze Mazingira ya tahadhari ya kujikinga kwa kunawa mikono au kutumia vitakasa mikono tunasisitiza hilo kila sehemu maofisi na sehemu zingine.
“Angalizo lingine kama huna ulazima wa kwenda sokoni usiende bora ubaki nyumbani ili kuepukana msongamano na kujilinda mwenyewe na kama huna ulazima wa kwenda sehemu yoyote ile bora ubaki nyumbani.
“Niseme tu hatuna taharuki kubwa lakini kuchukua tahadhari ni muhimu na ndio maana tumezuia mikusanyiko mikubwa lakini midogo tunawaambia wachukue tahadhari niwaambie tu wananchi kinga ni bora kuliko tiba,”alibainisha Dk. Ndugulile.