28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yapongeza hatua za mapambano dhidi ya UKIMWI

Na Mwandishi Wetu, Njombe

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu ), Balozi Pindi Chana amepongeza Mkoa wa Njombe kwa jitihada za kupunguza viwango vya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.

Waziri Pindi amesema hayo katika ziara yake Mkoani Njombe alipopokea taarifa ya Mkoa  kuhusu utekelezaji wa shughuli za UKIMWI na baadaye kutembelea vikundi vya wajasiriamali vya WAVIU, pamoja na kukagua ujenzi wa Kituo cha Care Treatment Centre (CTC), katika  Halmashauri ya Mji wa Makambako mkoani Njombe.

Mkurugenzi wa Tume ya kudhibiti UKIMWI(TACAIDS), Dk. Leonard Maboko akitoa Salamu katika Mkutano wa Nchi WAVIU mkoani Njombe.

Pindi alisema licha ya kupungua kwa maambukizi hayo bado ipo haja ya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili kudhibiti maambukizi mapya na wananchi kuwa katika hali ya usalama na afya bora.

“Nipongeze hatua hii kubwa mliyopiga kama Mkoa lakini tuna jukumu la kuendelea kupunguza viwango hivi na kama Serikali tumefanikiwa kupunguza maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa kina mama pia maambukizi ya virusi vya UKIMWI kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto,” amesema Pindi.

Vile vile alibainisha kwamba katika kuhakikisha vikundi vya ujasiriamali vya WAVIU vinaimarika kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali wanazozifanya kuendesha maisha na kupata huduma muhimu serikali imetenga asilimia 10 kwa ajili ya Vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kupata mikopo itakayowawezesha kuboresha shughul zao.

“Mashirikiano ya Serikali za mitaa na vikundi vya wajasiriamali  ni imara sana na niwasisitize mtumie fursa hii ya mikopo ambayo inatolewa na serikali yetu lengo ni kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma katika maendeleo na mtapata na elimu ya matumizi sahihi ya hiyo mikopo na ujasirimali,” ameeleza Pindi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu), Balozi Dk. Pindi Chana akiangalia Mradi wa kuku wa mayai alipotembelea kikundi cha WAVIU cha Juhudi mkoani Njombe.

Aidha alihimiza ushirikiano baina ya vikundi vya ujasirimali kushirkiana na serikali za mitaa katika maneo yao  ili  kupata taarifa za fursa mbalimbali pindi zinapojitokeza  katika maeneo yao huku akisisitiza WAVIU kujiunga katika  vikundi na kuendelea kuchapa kazi kwa manufaa yao na kuinua pato la Taifa.

Katika hatua nyingine Balozi Pindi alitoa wito kwa wananchi kutumia kituo kinachotoa huduma za afya cha  Care Treatment Centre (CTC) kujua hali ya afya zao akisema kuwa suala la  kujua hali  ya kiafya hususani  VVU ni jambo la msingi.

Naye Mkurugenzi wa Tume ya kudhibiti UKIMWI Tanzania ( TACAIDS), Dk. Leonard Maboko amesema mradi wa Southern Afrika Trade and Transportation Facilitation Project umehusisha ujenzi na ukarabati wa kituo hicho, maabara ya kupima virusi vya ukimwi, kutoa mashine za kupima virusi vya ukimwi na vichomea taka.

“Ujenzi huu pia umehusisha  ujenzi wa vituo 20 katika barabara kuu kutoka  Dar es salaam kuelekea mpaka wa Tunduma na Kasumulu  kwa ufadhili wa Benki ya Dunia kwa sababu ndio mwingiliano wa Tanzania na Nchi za Jangwa la Sahara ambazo kiwango cha maambukizi kiko juu  na vituo hivi vimejengwa katika vituo vya afya na vitakuwa chini ya Halmashauri,”amefafanua Dk. Maboko.

Akitaja mikoa mingine ambayo vituo hivyo vinajengwa ni pamoja na Mkoa wa Pwani wenye vituo vitano vya CTC, Mkoa wa Morogoro vituo vitatu, Mkoa wa Iringa vituo vinne, Mkoa wa Njombe wenye kituo kimoj pamoja na Mkoa wa Mbeya wenye vituo vitano na Mkoa wa Songwe  vituo viwili.

Akitoa neno la shukrani Mwenyekiti wa Jukwaa la Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI, Joseline Mtono ameishukuru Serikali na wadau mbalimbali wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na kuwajali watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI hali inayowafanya kujisikia nao ni sehemu ya jamii.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles