31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yafafanua uhaba wa dawa nchini

ummy-mwalimuNa ESTHER MNYIKA -DAR ES SALAAM

SERIKALI imetoa ufafanuzi wa upungufu wa  dawa  katika Bohari Kuu ya Dawa (MSD), huku ikikiri kukosekana kwa chanjo za watoto na wajawazito kwa kipindi cha miezi miwili.

Kauli ya serikali imekuja siku chache baada ya taarifa kusambaa katika vyombo vya habari ndani na nje ya nchi na kwenye mitandao ya kijamii, kwamba nchi inakabiliwa na uhaba wa dawa muhimu na chanjo katika Bohari Kuu ya Dawa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto, Ummy Mwalimu, alisema taarifa za ukosefu wa dawa si sahihi na zinalenga kupotosha umma na kuwatia hofu wananchi.

Hali ya upatikanaji wa dawa kwa sasa iko vizuri, dawa muhimu zinazohitajika sana nchini zinapatikana kwenye maghala ya MSD na kwa upande wa dawa za ‘antibiotics’ tuna amoxycillin, ciprofloxacin, cotrimoxazole na doxycycline.

“Kwa upande wa dawa za maumivu, tunazo za kutosha kama paracetamol, asprin na diclofenac  na pia tunazo dawa za malaria, kifua kikuu, ukoma na dawa za kufubaza makali ya Ukimwi.

“Kuhusu chanjo za watoto na wajawazito, ni kweli kulikuwa na uhaba nchini kwa kipindi cha miezi miwili iliyopita lakini sasa zinapatikana,” alisema Waziri Mwalimu.

Kwa mujibu wa waziri huyo, wiki iliyopita Serikali ilinunua na kupokea dozi milioni mbili za chanjo ya kifua kikuu, dozi milioni 1.2 za polio.

“Kwa hiyo, baada ya dozi hizo kuwasili nchini, sasa zinasambazwa katika vituo vya afya nchini.

“Pamoja na hali hii, changamoto kubwa  tunayokabiliana nayo ni kwamba kuna vituo vya afya, zahanati na hospitali haziagizi dawa MSD kwa wakati hali inayosababisha  kukosekana kwa dawa katika maeneo hayo,” alisema.

Kuhusu bajeti, alisema bajeti iliyotengwa kwa ajili ya  kununulia dawa  na vifaa tiba kwa mwaka wa fedha  2016/17 ni Sh bilioni 251 ikiwa ni tofauti na mwaka wa fedha 2015/16 zilipotengwa Sh bilioni 30.

Akizungumzia deni la MSD, alisema Serikali imedhamiria kulilipa kwa kuwa katika mwaka huu wa fedha, zimetengwa Sh bilioni 85 kwa ajili hiyo.

Katika maadhimisho ya Siku ya Afya ya Akili Duniani  ambayo kitaifa ilifanyika jana mkoani Dodoma, Waziri Mwalimu alisema afya ya akili bado ni tatizo nchini kwa kuwa kila wananchi wanne, mmoja kati yao anaugua ugonjwa wa akili.

“Waaguzi wa kugawa dawa bado ni tatizo hivyo tunatarajia kupeleka wauguzi kwa ajili ya kutoa huduma kwa wagonjwa hao,” alisema,”alisema.

Naye Mkurungenzi Mtendaji wa MSD, Laurean Bwanakunu, alisema dawa muhimu   hupatikana saa 24.

Aidha, alizitaka hospitali zote ambazo hazina dawa na chanjo, zipeleke maombi MSD ili waweze kupatiwa dawa hizo kwa haraka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles