33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yaagiza kufuta leseni 500 za madini

Na Seif Takaza, Singida

SERIKALI imeagiza Tume ya Madini kufuta leseni za utafiti wa madini zaidi ya 500 ambazo hazifanyiwi kazi wilayani Iramba mkoani Singida.

Agizo hilo limetolewa mwishoni mwa wiki na Naibu Waziri wa Madini, Dk. Lemomo Kiruswa katika kongamano la madini lililofanyika wilayani Iramba lililoandaliwa na ofisi ya Mkuu wa Wilaya Iramba Mkoani Singida.  

Dk. Kiruswa amesema wamiliki wa leseni za madini pamoja na wenye leseni za utafiti wa madini ambao hawazifanyii kazi kwa nchi nzima wajiongeze na kuanza mara moja kuzifanyia kazi kabla ya wizara hiyo haija chukua hatua za kuwafutia.

Amesema wilaya ya Iramba ina jumla ya leseni 694 za uchimbaji mdogo lakini ni 102 pekee ndizo zinazofanya kazi, leseni za uchimbaji wa kati zikiwa tano (MLs) ambapo nne zinana kampuni ya Sunshine ya Kichina ya Mining Ltd ambayo imeanza kuzalisha tangu Desemba 2021 na hadi kufikia Januari 2022 imeweza kuzalisha kilo 23.4 za dhahabu yenye ubora wa juu.

Amesema kutokana na uzalishaji huo Serikali kuu ilipata jumla ya Sh milioni 200 ikiwa ni mrabaha na ada ya ukaguzi na Halmashauri ya Iramba ilipata Sh milioni 10 ambapo pia ina leseni za utafiti wa dhahabu na almas (13) na leseni za uchenjuaji wa dhahabu 26.

Kufuatia kwa wamiliki wa leseni hizo ambazo hazifanyiwi kazi Dk. Kiruswa ameiagiza Tume ya Madini kianza zoezi la kuzifuatilia leseni hizo ambazo wahusika wamezishikilia ili utaratibu wa kuzifuta uweze kufanyika ziwe huru kwa kuwapatia watu wengine wenye nia ya kufanya kazi na Serikali iweze kupata mapato.

Aidha Dk. Kiruswa alitumia nafasi hiyo kumpongeza Mkuu wa wilaya hiyo Suleiman Mwenda kwa kuwa wa kwanza mkoani hapa kuandaa kongamano la namna hiyo na akaomba na mkoa nao ufanye hivyo jambo litakalosaidia kuwaunganisha wadau wote wa sekta ya madini mkoani hapa.

“Niseme ukweli tu kuwa wewe Mwenda ni DC pekee ndani ya Mkoa wa Singida na Tanzania kwa ujumla kufanya kongamano kubwa la namna hii lenye lengo la kuinua uchumi wa wananchi wa Iramba na Taifa kwa ujumla,” amesema Kiruswa.

Kwa upande wake Mwenda akitoa taarifa ya uchimbaji wa madini katika wilaya hiyo alisema akiwa msimamizi mkuu wa masuala ya uchumi na maendeleo hasa katika sekta ya madini mapato mchango wake ulikuwa ni mdogo sana.

“Kwa mwaka 2018/2019 mapato yao yaliyotokana na madini yalikuwa ni Sh milioni 15 na mwaka 2020/2021 baada ya kutembelea kwenye migodi ili kujionea kazi za uchimbaji na changamoto zilizopo mapato yaliyopatikana ni Sh bilioni 66,” alisema Mwenda. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Javan Diamonds Project (JDP) inayojishughulisha na Utafiti wa Almasi, Javan Bidogo ambaye pia ni mmiliki wa mradi wa utafutaji wa Almasi katika Kijiji cha Mbereseke kilichopo wilaya humo akitoa taarifa ya mradi huo kwenye kongamano hilo alisema kampuni yao ambayo ni ya wazawa imejikita kufanya utafiti wa Almasi katika wilaya za Ikungi na Iramba tangu mwezi Machi mwaka juzi na kuwa wapo katika hatua nzuri ya utafiti.

“Tumefanya uvumbuzi katika baadhi ya miamba inayokuwa na Almasi jumla yake ipo 13 na kati ya hiyo tisa ni mikubwa ambayo tumekuwa tukiifatilia sana,” alisema Bidogo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles