31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

SERIKALI KUTOA MAJIBU SAKATA LA MAFUTA KESHO

Gabriel Mushi, Dodoma

Serikali imeliomba Bunge kuridhia taarifa kamili ya uchunguzi wa kisayansi kuhusu mafuta ya kula yaliyopo kwenye meli zilizokwama bandarini, itolewe kesho baada ya kikao kinachoongozwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kukamilika.

Ombi hilo limetolewa jioni hii bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenister Mhagama baada ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kumuita ili atoe taarifa kuhusu maelekezo ya Bunge yaliyotolewa mapema asubuhi dhidi ya wizara ya viwanda, biashara na uwekezaji.

“Mheshimiwa Spika, tulipokea maelekezo yako, tulifanyia kazi kama ulivyotulekeza, kikao cha kupokea matokeo ya uchunguzi wa kisayansi kutoka katika taasisi husika zote kinaendelea na kinaongozwa na Waziri Mkuu na baada ya kikao hicho kukamilika tunaomba bunge liridhie taarifa ya serikali itolewe kesho jioni ili iwe taarifa kamilifu ya kutoa kuhusu mwelekeo wa kutatua tatizo hilo kutoka serikalini,” amesema Jenista.

Majibu hayo yaliyonekana kutomridhisha Spika Ndugai ambaye alizungumza kwa sauti ya ukali na kutoa tena maelekezo kwa serikali kuwa majibu hayo yatolewe kesho saa 11 jioni kabla ya kuendelea na shughuli nyingine ndani ya Bunge.

“Hilo wabunge sitawahoji… ni la utawala tu, tumepokea maelezo haya na tunayakubali kwa jambo moja kuwa kesho saa 11 kamili jioni tutaanza na hili, Mheshimiwa  Waziri Mwijage kesho saa 11 jioni tunaanza na hili, kama serikali haitakuwa na maelezo hadi kesho saa 11 kamili jioni basi mimi nitalifunga kiaina, tutawaachia Watanzania,” amesema Spika Ndugai.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles