24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali kuendelea kuboresha raslimali za gesi

*Lengo ni kuwapunguzia mzigo Watanzania

Na Beatrice Kaiza, Mtanzania Digital

SERIKALI imesema itaendelea kuboresha rasilimali za nishati hasa ya gesi za ndani ambazo zitapunguza gharama na kukuza matumizi ya huduma hiyo nchini na kuongeza ufanisi wa katika kukuza pato la Mtanzania mmoja mmoja na la Taifa kwa ujumla

Hayo yameelezwa leo Jumatano Machi 15, 2023 jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba katika Kongamano la Wadau wa Gesi LPG Afrika Mashariki 2023 ambapo amesema kuwa litasaidia kukuza ushiriki wa sekta binafsi katika kukuza sekta ya nishati nchini.

“Bila shaka maonyesho haya yatakuwa jukwaa muhimu katika kuongeza uelewa na kukuza uwekezaji katika sekta ya nishati hasa katika sekta ya LPG nchini Tanzania.

“Ni dhahiri kwamba mkusanyiko huu pia utawezesha wadau wote wakuu wa sekta ya LPG kujadili maoni yao na kushiriki masuala kuhusu mitindo ya biashara ya LPG nchini na duniani kote,”amesema Mramba.

Aidha, amesema kuwa Serikali inatekeleza majukumu yake kikamilifu katika kuhimiza utunzaji wa mazingira na afya za watanzania kwa kutoa elimu hali inayosaidia kupunguza matumizi ya kuni na kuhimiza matumizi ya LPG kama nishati mbadala ya kupikia majumbani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa LPG Tanzania, Amos Mwansumbue amesema asilimia kubwa ya mitungi ya gesi tunayotumia inatoka nje, bado hakujawa na viwanda vya kutosha vya kuzalisha mitungi hiyo hivyo wadau kutoka nje ambao wanajishughulisha na utengenezaji wa mitungi hiyo wamealikwa katika maonyesho hilo kuja kushiriki na kuleta ujuzi zaidi wa mitungi hiyo.

“Kongamano hilo linaloendelea linahusiana na biashara ya LPG, limeratibiwa na kampuni inayoitwa LPG Expo kutoka Singapore, watu kutoka nchi mbalimbali wamealikwa ambao wanajihusisha na biashara ya LPG duniani kote wakiwemo watengeneza mitungi ya gesi kutoka nchi mbalimbali ikiwemo Japan, Indonesia, Uturuki,” amesema Mwansumbue.

Ameongezea kuwa katika kongamano hilo kuna waelimishaji ambao wamekuja kuwaelimisha watanzania juu ya gesi yenyewe ya LPG kwa kutoa mifano kutoka nchi tofauti tofauti Duniani ambayo wameendelea kutumia gesi ambapo mifano hiyo inawasaidia watanzania kuboresha biashara ya gesi nchini.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Taifa Gesi, Hamisi Ramadhani amesema katika kongamano hilo ambalo pia linaenda sambamba na maonyesho ya bidhaa za gesi wanapata nafasi ya kuangalia teknolojia zilizopo ambazo zinaweza zikatumiwa na makampuni na wananchi kuweza kuendeleza matumizi endelevu ya gesi lakini pia kushiriki mjadala ambao watabadilishana mawazo namna ambavyo wanaweza wakakuza matumizi ya Gesi nchini ili kuweza kuachana na madhara ya matumizi ya mkaa na kuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles