33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali kuboresha masilahi ya watoa huduma sekta ya afya

upasuajiNa CLARA MATIMO-MWANZA

SERIKALI imeshauriwa kuboresha masilahi ya watoa huduma za afya ili wafanye kazi kwa moyo na kuepuka kukimbilia nje ya nchi kutafuta masilahi mazuri zaidi.

Wakizungumza katika semina ya haki afya na jinsi ya kuwasilisha malalamiko  kwa njia ya ujumbe mfupi kupitia simu ya kiganjani iliyoandaliwa na Tume ya Haki za Binadamu  na Utawala Bora (THBUB) iliyokutanisha makundi mbalimbali kutoka Mkoa wa Mwanza juzi, baadhi ya washiriki walisema  endapo  Serikali itaboresha masilahi ya watoa huduma za afya, itapunguza tatizo la wataalamu wa afya kwa kiasi fulani na hivyo kuwashawishi wale walioko nje nao kurejea.

Mmoja wa washiriki hao, Fatuma Mnahwate, alisema huduma zimekuwa duni kutokana na madaktari wengi kukimbilia nje na kushauri iwapo wataboreshewa masilahi yao, wengi watabaki nchini.

“Ili kuboresha upatikanaji wa haki  afya, pia Serikali ifanye ukaguzi wa mara kwa mara katika vituo vya kutoa huduma  za afya hasa vijijini ambako wananchi wengi wanaishi huko  na adhabu kali zitolewe kwa wafanyakazi wanaoenda  kinyume na maadili ya kazi zao,” alisema Fatuma Mnahwate.

Kwa upande wake, Mtafiti kutoka Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR),  Julius Siza, alisema asilimia 40 ya madaktari wanaishi na kufanya kazi nje ya nchi, hali inayozorotesha utoaji wa huduma.

Akizungumza na MTANZANIA, Mratibu wa Mifumo ya Habari na Mawasiliano  wa THBUB,  Wilfred Warioba, alisema lengo la semina hiyo  ni kuwezesha makundi maalumu kupata elimu ya haki afya na kujua jinsi ya kuwasilisha malalamiko katika ofisi zao  kwa njia ya ujumbe mfupi.

Alisema wametoa semina hiyo  kupitia Mradi  wa  Matumizi ya Teknolojia ya simu ya kiganjani katika kuwasilisha malalamiko THBUB   kwa ufadhili wa  Shirika la Misaada la Sweden (Sida) kupitia   Mtandao wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika kukuza demokrasia kwa njia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT For Democracy East Africa).

“Tulianza kuutekeleza mradi huu mwaka 2013, tunatarajia kuukamilisha mwaka huu, hadi sasa tumepata mafanikio mengi  ikiwamo kuwafikia watu wengi hasa   vijana,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles