23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

SEIF KHATIBU AJIVUNIA UADILIFU WAKE

Na RAMADHAN HASSAN-DODOMA


ALIYEKUWA Katibu wa NEC Idara ya Oganaizesheni ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mohammed Seif Khatibu, amefunguka na kusema anajivunia kuondoka katika nafasi hiyo akiwa msafi.

Alisema mpaka anaondolewa katika nafasi hiyo hana doa wala kasoro na kusisitiza kuwa katika chama ukifuata maadili utakuwa salama.

Khatibu ni mmoja kati ya viongozi watatu walioondolewa katika uongozi, ambapo nafasi yake kwa sasa inaongozwa na Pereira Ame Silima.

Viongozi wengine wapya ni Katibu wa NEC Uchumi na Fedha, Dk. Frank Haule na Naibu Katibu Mkuu CCM Zanzibar,  Abdallah Juma Abdallah.

Akizungumza katika kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), ambapo alikuwa akimwakilisha  Katibu Mkuu Abdulrahman Kinana, Khatibu alisema amekitumikia chama kwa takriban miaka 20 hivyo anakijua kinagaubaga.

Kikao hicho ambacho kiliongozwa na Mwenyekiti wa muda, Fatma Said Ally aliyepitishwa na wajumbe kuongoza kikao baada ya aliyekuwa mwenyekiti wa umoja huo, Sophia Simba kuwa miongoni mwa waliovuliwa uanachama.

Alisema watu wote waliopewa adhabu ndani ya chama ikiwamo kufukuzwa uanachama, wamepata ajali ya kisiasa ambayo haiangalii kama ni mwanamume au mwanamke, mkubwa au mdogo.

“Wote  waliopewa adhabu ikiwamo ya kufukuzwa uanachama na kupewa onyo, wameadhibiwa kutokana na kuendelea na makundi mengine hata pale ambapo chama kilikuwa kimeshapata mgombea wake,” alisema.

Kwa upande wake, Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi wa Chama hicho, Humphrey Polepole, alisema kupitia mageuzi yanayofanyika ndani ya chama watahakikisha wanatoa kipaumbele kwa wanawake kutokana na kwamba nchi haiwezi kupiga hatua bila ya mwanamke.

Polepole alisema Tanzania na nchi nyingine za Afrika bado zinaendeleza mfumo dume lakini kutokana na mageuzi yaliyofanyika katika chama itarekebisha hali hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles