27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Saudi Arabia kuwekewa vikwazo

PARIS, UFARANSA



UFARANSA na Ujerumani zimetangaza kuwa zitaiwekea vikwazo Saudi Arabia kuhusiana na mauaji ya mwandishi wa habari, Jamal Khashoggi.

Mataifa hayo na mengine ndani ya Umoja wa Ulaya (EU), yamekuwa yakiitaka nchi hiyo kuanika ukweli wa kilichojiri hadi kuuawa kwa mwandishi huyo mkosoaji mkubwa wa utawala wa Kifalme wa Saudi Arabia hasa  Mrithi wa Kiti cha Ufalme, Mohammed bin Salman.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa, Jean-Yves Le Drian, amesema wanapanga kuiwekea vikwazo Saudi Arabia na juu ya hilo wanataka lazima ukweli wote uanikwe kuhusu kuuawa kwa Khashoggi.

Saudi Arabia ni mojawapo ya mteja muhimu katika sekta ya ulinzi ya Ufaransa, ambako mwaka jana ilinunua silaha zenye thamani ya Euro bilioni 1.38 kutoka Ufaransa.

Ujerumani, ambayo ilitangulia kusimamisha mauzo ya silaha kwa taifa hilo baada ya ukweli wa mauaji hayo kuanikwa, kwa upande mwingine, imetangaza kuwawekea vikwazo raia 18 wa Saudi Arabia wanaoshukiwa kuhusika na mauaji ya Khashoggi.

Hata hivyo, Rais Donald Trump wa Marekani ameenda tofauti na washirika wa Ulaya kwa kuchagua kuikingia kifua Saudi Arabia.

Rais Trump, ambaye amekuwa akiisifu Saudi Arabia  kuwa ni mshirika mzuri kabisa wa nchi yake, anabanwa  ndani ya nchi yake na chama chake  cha Republican pamoja na Democrat aichukulie hatua kali nchi hiyo.

Saudi Arabia imepinga ripoti zinazodai Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) limesema mwanamfalme Mohammed bin Salman ndiye aliyetoa maagizo ya kuuawa kwa Khashoggi katika ubalozi mdogo wa Saudi Arabia nchini Uturuki.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia,  Adel al Jubeir amesema ufalme wa nchi hiyo unajua kwamba madai hayo   hayana ukweli na wanayapinga wakisisitiza hawataruhusu katu majaribio ya kuuhujumu uongozi wa taifa kwa namna yoyote na kutoka kwa mtu yeyote.

Al Jubeir pia ameongeza kusema kwamba haki katika kisa cha kuuawa Khashoggi ni kitu cha kwanza ambacho Saudi Arabia inakitaka kabla hata ya Jumuiya ya kimataifa kuibana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles