24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Samatta asaini miaka minne Aston Villa

Mohamed kassara-Dar es salaam

HATIMAYE, nahodha wa timu ya Taifa Tanzania, ‘Taifa Stars’ Mbwana Samatta amekamilisharasmi uhamisho wake wa kujiunga na klabu ya Aston Villa  ya England kwa mkataba wa miaka minne na nusu utakaomfanya kuichezea timu hiyo hadi Juni 2024.

Samatta anatua Villa kwa dau la Pauni  milioni 10 (Sh Bilioni 30 za Tanzania) akitokea KRC Genk ya Ubelgiji, aliyoisadia kutwaa ubingwa msimu uliopita na kukata tiketi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Kilichokuwa kikisubiriwa kwa hamu ni Villa kutangaza rasmi usajili huo, baada ya Samatta kukamilisha taratibu zote za usajili, ikiwemo kufuzu vipimo vya afya tangu Ijumaa iliyopita.

Samatta atakuwa mchezaji watatu kujiunga na timu hiyo katika kipindi hiki cha dirisha dogo la usajili, baada ya mlinda mlango wa zamani wa Liverpool, Pepe Reina akitokea AC Milan ya Italia na kiungo wa Chelsea, Danny Drinkwater wote wakitua kwa mkopo.

Taarifa kutoka jijini Birmingham yaliko makazi ya Villa, zinaeleza kuwa Samatta, licha ya kukamilisha taratibu zote, kilichochelewesha kutangazwa kwa usajili wake kibali cha kufanya kazi England.

Villa ilikuwa na matumaini makubwa ya kukamilisha usajili huo mapema ili mshambuliaji huyo  auwahi mchezo wa Ligi Kuu England dhidi ya Watford uliochezwa jana , lakini hilo lilishindikanabaada ya kuchelewa kupata kibali hicho.

Hata hivyo, Samatta anatarajia kuanza kuichezea timu hiyo katika mchezo wa marudiano wa nusu fainali ya Kombe la Ligi dhidi ya Leicester City  utakaochezwa Jumanne ijayo kwenye Uwanja wa King Power.

Samatta anatarajiwa kuiongezea nguvu safu ya ushambuliaji ya Villa kipindi hiki ambacho inamkosa straika Wesley, ambaye ni majeruhi na anatakiwa kuwa nje ya dimba hadi mwishoni mwa msimu.
Baada ya klabu ya Aston Villa kutangaza kufanikisha uhamisho wa Samatta kupitia ukurusa wao wa mtandao wa kijamii wa Instagram, kocha wa kikosi hicho, Dean Smith alishindwa kuficha furaha aliyonayo kwa mchezaji huyo.

 “Nimefurahi mno kufanikiwa kumleta Mbwana katika klabu hii, amefunga mabao muda wote na ninasubiri kufanya naye kazi,”alisema kocha huyo.

Samatta kwa upande wake , alisema: “Ilikuwa ni ndoto, asante Aston Villa kwa kuifanya itimie, sasa ni wakati wa kujitoa kwa 100% kwa ajili ya timu, ndugu zangu Watanzania nawashukuru kwa maombi yenu, mapambano yanaendelea, haina kufeli,”alisema Samatta wakati akifanya mahojiano na chombo kimoja cha habari.

Mpachika mabao huyo wa zamani wa TP Mazembe ya Jamhuri Kidemokrasi ya Kongo (DRC) na Simba, hadi anaondoka Genk alikuwa ameichezea michezo 191, akifunga mabao 76 na kutoa pasi za mabao 20.

Msimu huu, aliifungia timu hiyo mabao 10, huku matatu akifunga katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya ya hatua ya makundi dhidi ya Liverpool na RB Salzburg ya Austria.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles