29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Salt Bae; Mchoma nyama tajiri anayevutia mastaa

CHRISTOPHER MSEKENA

*Awahudumia Messi, Pogba, Dj Khaled, Ben PolMWAKA 2008, huko nchini Uturuki kijana, Nusret Gökçe, aliiambia nafsi yake kuwa itakapofika 2010, atakuwa amefungua mgawaha wake wa chakula ili aweze kukuza jina lake dunia nzima.

Huyu ni Salt Bae, mchoma nyama tajiri mwenye mbwembwe aliyewahudumia mastaa wakubwa duniani kama Lionel Messi, Paul Pogba, French Montana, Dj Khaled, Drake, David Beckham, Karim Benzema, Franck Ribery, Diego Maradona na wengine wengi.

Wiki hii pia staa wa Bongo Fleva, Ben Paul naye alipata bahati ya kuhudumiwa na Salt Bae katika mgahawa wake wa Nusr-Et, uliopo Dubai alipokuwa matembezini na mpenzi wake, Anerlisa.

SALT BAE NI NANI?

Mchoma nyama huyu alizaliwa miaka 36, iliyopita mjini Erzurum huko Uturuki katika familia ya baba anayeitwa Faik Gokce na mama Fatma, yenye jumla ya watoto wanne huku mzee wake akiwa mfanyakazi katika moja ya migodi nchini humo.

Uchumi wa familia yao uliyumba hali iliyosababisha Salt Bae aahirishe masomo yake akiwa darasa la sita na kuingia mtaani kutafuta fursa nyingine za kujitengenezea maisha bora  ambapo alikwenda kufanya kazi katika bucha ya nyama huko Kadikoy mjini Instanbul.

AINGIA RASMI KWENYE BIASHARA

Ilipofika mwaka 2007, aliondoka Uturuki na kwenda Argentina na Marekani, huko alifanya kazi kwa kujitolea katika migahawa mbalimbali ya kiwango cha chini, lengo likiwa ni kupata maarifa zaidi ya kuandaa vyakula na namna ya kuendesha biashara hiyo.

Salt Bae, alikaa Marekani mpaka 2010 na kurudi tena Uturuki ambako alifanikiwa kufungua mgahawa wake wa kwanza mjini Instanbul. Aliuendeesha kwa mafanikio makubwa mpaka akafungua mgahawa mwingine huko Dubai ambao ndiyo huo Ben Paul na mpenzi wake alikwenda kupata chakula.

MBWEMBWE ZAMPA UMAARUFU

Naweza kusema Salt Bae ni mchoma nyama mwenye mbwembwe nyingi pale anapoandaa kilaji na siyo kila mteja anaweza kupata bahati ya kuhudumiwa naye bali ni wale mastaa na watu wenye hadhi ya juu. Utavutiwa na mikogo ya Salt Bae pale anapoanza kukata nyama, kuchoma na kumwandalia mteja mezani.

Mwaka 2017, Salt Bae alionekana katika video iliyosambaa mtandaoni na kutazamwa mara milioni 10 katika mtandao wa Instagram akikata nyama kwa madoido na kuinyunyizia chumvi kwa mtindo wa kipekee (Unachukua chumvi mkononi unakunja mkono mfano wa nyoka na kuiachia kwenye nyama).

MIGAHAWA SEHEMU MBALIMBALI

Salt Bae ni bosi wa migahawa ya Nusr-Et ambayo ipo katika miji mbalimbali kama vile Uturuki, Dubai, Abu Dabi, Miami na New York huko Marekani, Doha (Qatar) na hivi karibuni amepanga kutoa huduma ya nyama choma dunia nzima.

Mbali na migawaha hiyo, Salt Bae anamiliki mashamba ya mifugo katika miji mbalimbali kama Sicily, Italia, Bogota, Colombia, Karanlikidere na Topuk huko Uturuki.

ANA UTAJIRI WA KUTOSHA

Mchoma nyama huyu ana mkwanja wa kutosha, utajiri uliotokana na migahawa hiyo. Mpaka mwaka jana mwezi Julai, Salt Bae  alikuwa na utajiri wa dola za kimarekani 50,000,000 ambazo ni zaidi ya bilioni 114.9.

MBALI NA BIASHARA

Licha ya kufanya kazi saa 18 kwa siku, Salt Bae, amekuwa akipenda michezo na shughuli zingine nje ya biashara ya chakula. Jamaa anapenda kucheza na wanyama wa nyumbani kama vile mbwa na farasi pia anafanya michezo ya masumbwi na soka.

FAMILIA

Salt Bae, bado hajafanikiwa kufunga ndoa lakini mpaka sasa ana watoto tisa ambao amezaa na wanawake tofauti tofauti ambao anawapenda na ameendelea kuwa nao karibu kwa matunzo na mapenzi kama baba bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles