Christopher Msekena
SALLAM Sharaff maarufu kama Sallam Sk ambaye ni meneja wa Diamond Platnumz na rapa Hamis Mwinjuma ‘Mwana Fa’, wamekutwa na maambukizi ya virusi vya corona na sasa wapo chini ya uangalizi.
Hatua ya kutangaza majibu ya vipimo yao ya corona yamekuja baada ya kusambaa kwa tetesi kuwa wawili hao wanaumwa, ndipo jana kila mmoja kwa wakati wake akatangaza kuathirika na virusi hivyo.
“Napenda kuwajulisha na kuwatoa hofu ndugu, jamaa na marafiki kuwa nimepata majibu ya vipimo na nimeonekana nikiwa na corona virus, kwa sasa nipo chini ya uwangalizi mzuri na afya yangu inaendelea vizuri pia naishukuru Serikali kwa maandalizi mazuri na huduma ninayopata wodini, toka juzi nipo mwenyewe,” alisema Sallam.
Siku kadhaa zilizopita, Sallam na Diamond Platnumz alikuwa kwenye ziara mjini Zurich, Switzerland katika makumbusho ya Shirikisho la Soka duniani (FIFA)
Naye Mwana Fa alisema: “Nilipima corona jana (juzi) na leo vipimo vimerudi vipo chanya, nilitoka safari juzi Afrika Kusini joto langu la mwili likawa halieleweki, kwasababu habari kubwa ni corona nikawa nimejitenga ili nisiathiri watu wengine, bado nimetengwa, ugonjwa upo kweli na unaweza ukampata mtu yeyote mimi nipo vizuri siumwi chochote,” alisema Mwana Fa.