26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

SAKATA LA UDA LAMPELEKA MEYA DODOMA

Na NORA DAMIAN-DAR ES SALAAM

SAKATA la fedha za mauzo ya hisa za Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zilizokuwa katika Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), limechukua sura mpya baada ya Meya wa jiji hilo, Isaya Mwita kuamua kwenda Dodoma kukutana na wabunge wa mkoa huo.

Wiki iliyopita wakati akizindua awamu ya kwanza ya mradi wa mabasi yaendayo haraka (UDART), Rais Dk. John Magufuli, alitoa siku tano kwa Jiji la Dar es Salaam kufanya uamuzi juu ya matumizi ya Sh bilioni 5.8 zilizotolewa na mbia anayemiliki asilimia 51 ya hisa za Kampuni ya UDA-RT.

Jumatatu wiki hii ndiyo ilikuwa siku ya tano kulingana na agizo la Rais Magufuli, lakini jiji hilo bado halijawasilisha mapendekezo yake.

Chanzo cha kuaminika kililiambia MTANZANIA kuwa wabunge wanaotoka Mkoa wa Dar es Salaam walikuwa na kikao na Meya Mwita wakijadili kuhusu suala hilo.

“Meya yuko Dodoma na amekuja kwa ajili ya suala hilo… amekutana na wabunge,” kilisema chanzo hicho.

Alipoulizwa Meya Mwita hakukubali wala kukataa, badala yake alimtaka mwandishi kuwa na subira hadi kesho (leo) atakapoeleza uamuzi uliofikiwa.

“Nani kakuambia niko Dodoma… mimi ni Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dodoma nimefuata nini? Inaonekana una vyanzo vingi sana.

“Nakuomba kama utakubali unitafute kesho jioni nitaweza kusema chochote, nitakuwa nimejua ‘the way forward’ (mwelekeo)… Lakini mtuombee kwa sababu changamoto ni nyingi,” alisema Mwita.

Wiki iliyopita wakati wa kikao cha dharura cha Baraza la Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam, walishindwa kuafikiana juu ya fedha hizo zitumike au zisitumike na kuamua kupiga kura ambayo matokeo yalikuwa sare.

Hatua hiyo ikamlazimu Meya Mwita kupiga kura ya turufu ambayo aliungana na upande uliokataa fedha hizo zisitumike.

Baada ya kikao hicho, Meya Mwita aliwaeleza waandishi wa habari kwamba watamwomba Rais Magufuli awaongezee muda ili waweze kujadiliana zaidi.

Meya huyo aliainisha sababu kadhaa zikiwamo za kutokuwapo kwa wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam na kwamba katika kikao hicho Mbunge wa Temeke, Abdallah Mtolea (CUF), ndiye pekee aliyekuwapo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles