27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Safari ya Sumaye katika siasa

Mwandishi wetu –Dar es salaam

FREDERICK Sumaye amekuwa mwanasiasa kwa muda mrefu akiwa amefanikiwa kushika nyadhifa mbalimbali serikalini, na kufanikiwa kuwa waziri mkuu kwa miaka 10 katika Serikali ya awamu ya tatu, iliyoongozwa na Rais Benjamin Mkapa.

Kiongozi huyo aliyezaliwa mwaka 1950, alishika wadhifa wa waziri mkuu tangu alipoteuliwa na kutangazwa rasmi Novemba 28, 1995 hadi Desemba 2005.

Akiwa mwanachama wa CCM, Sumaye aliwahi kuwa Mbunge wa Hanang kwa miaka 22, kuanzia mwaka 1983 hadi 2005.

Kabla ya kuwa Waziri Mkuu, Sumaye alihudumu kama Waziri wa Kilimo, Mifugo na Ushirika katika Serikali ya awamu ya pili iliyokuwa chini ta Rais Ali Hassan Mwinyi, aliyeongoza kuanzia mwaka 1985 hadi 1995.

Baada ya kutoka madarakani, kuanzia mwaka 2006 Sumaye alirejea shuleni baada ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Harvard, kupitia programu ya Edward S. Mason kwenye shule maalumu ya John F. Kennedy iliyopo chuoni hapo, na alipata shahada ya juu katika Usimamizi wa Umma (Public Administration).

Alirejea nchini baada ya kumaliza masono yake na mwaka 2015 alijitokeza kuomba ridhaa ya kuteuliwa kupeperusha bendera ya CCM katika kiti cha urais, lakini hakufanikiwa.

Agosti 2015, muda mfupi baada ya kutoteuliwa na CCM, alijitoa katika chama hicho na kujiunga upinzani kupitia Chadema.

Alisema kuwa ameamua kujiunga na upinzani ili atumie uzoefu wake kuimarisha demokrasia nchini kwa kuweka nguvu upande wa pili, yaani upande we upinzani, ili kuwe na ushindani wenye nguvu zinazofanana.

Tangu wakati huo, amekuwa akisisitiza kuwa uwapo wa vyama vyenye nguvu zinazofanana unawapa wananchi uhuru wa kuchagua chama chochote kati ya hivyo vyenye nguvu kwa matumaini kuwa chama chochote kati ya hivyo kinaweza kuongoza nchi.

Alikuwa akisisitiza kuwa alihamia upinzani kuupa upinzani nguvu ya kushindana na CCM na itakuwa na manufaa makubwa kwa sababu CCM hawatalala usingizi kwa sababu chama chochote kitakachoshika madaraka kinajua kuwa kina miaka mitano tu ya uongozi.

Amekuwa akisisitiza kuwa chama tawala kiwe CCM, au Chadema au ACT Wazalendo au TLP kisipolala usingizi kikafanya kazi ipasavyo wanaofaidika ni wananchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles