Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital
Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) imelaani vikali mauaji ya wanajeshi wake yaliyofanywa na kundi la waasi la M23 mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). SADC imetaja mashambulizi hayo kama “kitendo cha uchokozi” kinachozidi kuzorotesha hali ya kibinadamu na usalama katika eneo hilo.

“Jaribio la M23 kupanua eneo lake kunazidisha hali ya kibinadamu kuwa mbaya zaidi mashariki mwa DRC,” SADC ilisema katika taarifa yake Jumamosi.
Ingawa jumuiya hiyo haikutoa takwimu rasmi za wanajeshi wake waliouawa au kujeruhiwa, nchi wanachama zimethibitisha vifo vya raia wao. Afrika Kusini ilitangaza kupoteza wanajeshi wake tisa, huku Malawi ikiripoti vifo vya raia wake watatu. Aidha, mwanajeshi mmoja kutoka Uruguay anayehudumu na ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani alipoteza maisha, na raia wengine wanne walijeruhiwa katika shambulio hilo, serikali ya Uruguay ilitangaza.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Jumamosi, msemaji wa jeshi la DRC, Jenerali Sylvain Ekenge, alisema: “Rwanda imedhamiria kuuteka mji wa Goma,” akihusisha mashambulizi ya hivi karibuni ya M23 na mipango ya Kigali.
Serikali ya Kongo na wataalamu wa Umoja wa Mataifa wameishutumu Rwanda kwa kuwaunga mkono waasi wa M23, lakini serikali ya Rwanda imeendelea kukanusha madai hayo mara kwa mara.
Katika hatua nyingine, Umoja wa Ulaya (EU) ulilaani kwa nguvu uwepo wa kijeshi wa Rwanda mashariki mwa DRC. Mkuu wa sera za kigeni wa EU, Kaja Kallas, alisema: “Rwanda lazima iache kusaidia M23 na kujiondoa. Hii ni ukiukaji wazi wa sheria za kimataifa, makubaliano ya Umoja wa Mataifa, na uadilifu wa eneo la DRC.”
SADC pia imetoa wito kwa pande zote zinazohusika katika mzozo huo kufuata sheria za makubaliano ya amani na kuonyesha nia ya kushiriki katika mazungumzo yenye lengo la kurejesha utulivu.
Wakati huo huo, Mkutano wa dharura wa Umoja wa Mataifa uliopangwa kufanyika Jumatatu kwa ajili ya kujadili hali ya Mashariki mwa DRC umehimizwa kufanyika Jumapili kutokana na kuzidi kwa mapigano, kwa mujibu wa vyanzo vya kidiplomasia vilivyonukuliwa na shirika la habari la AFP.