33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Rungu la wasaliti CCM lawaangukia vigogo

Na ABRAHAM GWANDU

-ARUSHA.

CHAMA cha Mapinduzi Mkoa wa Arusha inadaiwa kimewafukuza uanachama baadhi ya vigogo wake akiwamo Mwenyekiti wa chama hicho Wilaya ya Arusha,  Wilfred Soileli.

Wanachama hao wanatuhumiwa  kukisaliti chama hicho kabla na baada ya uchaguzi mkuu wakidaiwa kuwa wafuasi watiifu kwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.

Wengine waliotimuliwa ni   Mjumbe wa halmashauri kuu ya taifa kutoka jimbo la Arumeru Magharibi Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC ) na mfanyabiashara maarufu wa madini ya vito, Mathias Manga na Julius Mungure wa Jimbo la Arumeru Mashariki.

Wakati vigogo hao mkoani Arusha ikielezwa wamevuliwa uanachama wiki iliyopita, Kamati ndogo ya Maadili  ya CCM iliyokutana  Dodoma  iliwahoji wanachama wake ambao wanadaiwa kukisaliti chama hicho.

Hao ni Profesa Juma Kapuya, Nazir Karamagi   na Ally Sumaye ambao wote wanadaiwa kukisaliti chama wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Wana CCM hao waliohojiwa na kamati hiyo iliyoongozwa na Naibu Katibu Mkuu Bara, Rodrick Mpogolo, ambaye gazeti hili lilipomtafuta kwa   simu, haikupokewa.

Taarifa zilizosambaa   jijini hapa jana jioni zilidai  uamuzi wa kuwafukuza uanachama viongozi hao ulifanyika katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Mkoa wa Arusha kilichofanyika Jumamosi chini ya Mwenyekiti wa chama wa mkoa huo, Lekule Laizer.

Baadhi ya wajumbe wa kikao hicho waliiambia MTANZANIA kuwa Soileli na Manga walituhumiwa kushirikiana   kutoa siri na mikakati ya chama na kuipeleka kwa viongozi wa Ukawa hasa Lowassa ambaye alikuwa mgombea wa nafasi ya Rais.

“Hawa walionywa mara nyingi waache tabia ya kushirikiana na wapinzani hasa Lowassa lakini Manga aliwahi kusema yuko tayari kuchukuliwa hatua lakini asingeacha  urafiki wake na Lowassa kwani siasa siyo uadui,” alisema mmoja wa wajumbe wa kikao hicho ambaye hakutata kutwa jina lake gazetini

Gazeti hili lilimtafuta kwa njia ya simu Mwenyekiti Soileli  aweze kutoa ufafanuzi wa suala hilo.

Alisema kwa kifupi kuwa bado hajapata taarifa yoyote kuhusu kufukuzwa kwake.

Kwa upande wao wajumbe wa NEC  waliofukuzwa uanachama, Mathias Manga na Julius Mungure  simu zao hazikupatikana .

Akizungumzia taarifa hizo, Katibu wa Siasa na Uenezi wa Mkoa wa Arusha,  Shaban Mdoe, hakukataa wala kukubali ukweli wa taarifa hizo.

Alisisitiza kuwa chama hicho kitatoa ufafanuzi wa kina kuhusu kilichoamuliwa na kikao leo saa 6.00 mchana katika ofisi za CCM Mkoa.

“Siwezi kusema chochote kwa sasa kuhusu taarifa hizo mpaka kesho Jumatatu saa 6.00 mchana.

“Hizo tetetsi zinazosababisha maswali kuhusu uamuzi uliofikiwa na kikao cha Halmashauri Kuu ya Mkoa kilichoketi Jumamosi tutatoa ufafanuzi kesho Jumatatu (leo),” alisema Mdoe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles