31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Rugemarila , Seth waendelea kusota rumande

PATRICIA KIMELEMETA

UPELELEZI wa kesi ya uhujumu uchumi na utakatishaji wa fedha inayowakabili wafanyabiashara Herbinder Seth na mwenzake James Rugemarila, bado unaendelea na washtakiwa wanaendelea kusota rumande.

Washtakiwa hao kwa pamoja walisomewa mashtaka 12 ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha na Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai  katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi.

Wakili Swai alidai mahakamani hapo jana kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya kutajwa, lakini upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuiomba mahakama hiyo kupanga tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Baada ya kueleza hayo, Hakimu Shaidi aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 28, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.

Washtakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na mashitaka hayo 12 ya uhujumu uchumi  kwa kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu, kughushi nyaraka, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu,  kutakatisha fedha  na kuisababishia Serikali hasara ya Dola za Marekani  22, 198,544.60 na Sh 309,461,300,158.27.

Washtakiwa hao wanadaiwa kuwa Oktoba 18, 2011 na Machi 19 , 2014 jijini Dar es Salaam walikula njama katika nchi za Afrika Kusini, Kenya na India ili kutenda kosa.

Wanadaiwa katika mashtaka ya kujipatia fedha kwamba  kati ya  Novemba 28 na 29, 2011 na Januari 23,2014 katika makao makuu ya Benki ya Stanbic Kinondoni  na Benki ya Mkombozi Tawi la Mtakatifu Joseph,  kwa ulaghai washitakiwa hao walijipatia kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dola za Marekani  22,198,544.60 na Sh 309, 461,300,158.27.   

 Wanadaiwa kuisababishia Serikali hasara ambapo inadaiwa walitenda makosa hayo Novemba 29, 2013 katika Benki ya Stanbic tawi la  kati kinondoni, kwa vitendo vyao waliisababishia serikali hasara ya Dola za Marekani 22, 198, 544.60 na Sh 309,461,300,158.27.

Kati ya Novemba 29,2013 na Januari 23, 2014 maeneo tofauti Dar es Salaam kwa pamoja walitenda kosa la kutakatisha fedha kwa kuchukua fedha kutoka BoT ambazo ni Dola za Marekani milioni 22.1 na Sh bilioni 309.4  wakati wakijua fedha hizo ni zao la kujihusisha na genge la uhalifu.

Washitakiwa hao bado wanasota rumande kwa kuwa mashtaka hayo hayana dhamana kwa mujibu wa sheria.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles