33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

RIPOTI YA CAG YAIBUA UBADHIRIFU MPYA

Na ELIZABETH HOMBO -DAR ES SALAAM

MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad, amewasilisha kwa Rais Dk. John Magufuli, ripoti yake ya mwaka 2016/17, huku akigusia baadhi ya madudu yaliyomo.

Akitoa mchanganuo wa hati za ukaguzi wa hesabu katika Serikali Kuu na taasisi zake, alisema ofisi yake imetoa jumla ya hati 561.

Profesa Assad alisema kati ya hati hizo, 502 sawa na asilimia 90 zinaridhisha, 45 sawa na asilimia 8 zina shaka, 7 sawa na asilimia 1 haziridhishi na 7 sawa na asilimia 1 ni mbaya.

Alisema mashirika ya umma yamepata hati safi kwa asilimia 96, Mamlaka ya Serikali za Mitaa asilimia 90 na Serikali Kuu asilimia 86.

Kuhusu deni la taifa, alisema linatia wasiwasi na kuishauri Serikali kuchukua hatua kupunguza ukubwa wake.

Profesa Assad alisema deni hilo limekua kutoka Sh trilioni 41 hadi 46 mwaka uliopita.

“Deni la taifa limekua kwa Sh trilioni 5 sawa na asilimia 12. Tulichosema hapa, kweli ukuaji wa deni tunasema ni himilivu, lakini jinsi ‘volume’ inavyoongezeka tunakaribia maeneo ya wasiwasi.

“Asilimia 72 ya pato la taifa (GDP) si mbaya, lakini ikifika asilimia 76, nchi nyingine zimepata shida. Inabidi tuangalie namna gani ambayo tunaweza ku-‘control’ ukuaji wa deni la taifa,” alisema Profesa Assad.

 

SERIKALI KUU

Mdhibiti huyo alisema eneo la kwanza kwa upande wa Serikali Kuu ni kuhusu makusanyo ambako kwa upande Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wamebaini mapungufu katika kesi za muda mrefu kwenye mahakama za rufaa na kodi ambazo zinafikia Sh trilioni 4.4.

Alisema eneo jingine ni mapungufu katika kushughulikia pingamizi za kodi ambazo zinafikia Sh bilioni 739.

“Eneo jingine la tatu; tulizungumzia mifumo ambayo hairidhishi katika udhibiti wa mizigo ambayo inapita nchini kwenda nchi nyingine.

“Kwamba kulikuwa kuna lita milioni 26 ambayo kodi yake ilikuwa inafika Sh bilioni 14 ambayo mafuta hayo hayakusafirishwa kwenda nje, yalitumiwa ndani ya nchi kinyume na sheria.

“Nne; kuna mitambo ya uchenjuaji wa madini katika mikoa ya Mwanza, eneo la Kahama na maeneo ya Shinyanga inayofikia 84 ambayo inafanya kazi bila leseni, hivyo inasababisha ukosefu mapato katika Serikali wa Sh bilioni 232,” alisema.

 

MATIBABU NJE YA NCHI

Profesa Assad alisema malipo ya matibabu nje ya nchi, hasa India, kwa mwaka huu yamefikia karibu Sh bilioni 46.

“Hizi fedha ni nyingi sana kama hakuna mpango wa kulipa kidogo kidogo. Tulikuwa tunashauri Serikali iweke eneo hili kama eneo muhimu kulipa deni hili, kwa sababu mwisho tunaweza kunyimwa huduma kabisa. Kila mwaka tulipe deni hili,” alisema.

 

USIMAMIZI MIKATABA

Profesa Assad alisema ripoti yao imebaini udhaifu wa usimamizi katika mikataba ya manunuzi katika Serikali Kuu, ambako taasisi saba zilifanya manunuzi na kufikia Sh bilioni tatu bila kuidhinishwa na bodi.

“Na taasisi 11 zilinunua bidhaa na huduma za ujenzi ambazo zinafikia Sh bilioni 1.5, kutoka kwa wazabuni mbalimbali bila kuwa na mikataba kinyume na kanuni ya 10 ya manunuzi ya umma ya mwaka 2013.

“Pia kuna taasisi 14, zilikaguliwa ambazo zilinunua na kupokea bidhaa zenye thamani ya Sh bilioni 1.7 bila kukaguliwa na kamati zinazohusika.

“Taasisi nyingine nane tulibaini kuna manunuzi ya vifaa ya Sh bilioni 53, ziliagiza na kununua, lakini havikupokewa,” alisema Profesa Assad.

 

MADUDU NSSF

Profesa Assad alisema ripoti yake pia imebaini udanganyifu katika mkopo wa Sh bilioni 7 uliotolewa na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwenda taasisi nne ambazo hazikutajwa majina.

Alisema mkataba wa utoaji mkopo huo unaonyesha Sh bilioni 60 zilitakiwa kutolewa, lakini NSSF ikaongeza Sh bilioni 7 nje ya mkataba husika.

“Mkataba ulisema mkopo utakuwa ni Sh bilioni 60, lakini ililipa Sh bilioni 67, kwahiyo ililipa ziada ya Sh bilioni 7 bila kuwa na mkataba.

“Kwahiyo kuna wasiwasi huenda hizo fedha zikapotea,” alisema.

 

MSD

Profesa Assad alisema katika ukaguzi wao, wamebaini kulikuwa na dawa zilizopitwa na muda zinazofikia Sh bilioni 4.5.

“Hili tuliona ni tatizo. Mimi huwa najiuliza kwanini Wahindi hawana ‘expire drugs’ nyingi? Kwanini MSD inakuwa na ‘expire drugs’ nyingi?

“Lakini ukiwa na ‘system’ ya ‘store control’ nzuri unajua mwezi ujao au miezi miwili ijayo madawa yangu yata-‘expire’, unatoa ‘promotion’ watu wananunua unapata hasara kidogo kuliko kupoteza yote, kuliko ukisubiri muda wake wa kuharibika,” alishauri.

 

TRA HAIKULIPA RAHCO

Profesa Assad alisema wamebaini TRA haikulipa mapato ya reli yaliyofikia kiasi cha Sh bilioni 94 katika Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO).

Alisema mapato hayo yalitakiwa kwenda RAHCO, lakini hayakufikishwa hadi leo.

Profesa Assad alisema ukaguzi mwingine wa RAHCO unaonyesha kufanyika kwa upembuzi yakinifu kwa gharama ya Sh bilioni 20 bila kuwa na utekelezaji wa mradi ambao hakuutaja baada ya kukosa fedha.

Alisema hatua ya kufanya upembuzi yakinifu bila kutekeleza mradi ni upotevu wa fedha.

 

MADUDU CHAMA CHA WALIMU

Profesa Assad alisema ripoti yao imebaini madudu katika ukaguzi wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) ambako kuna mambo yanafanywa kinyume cha matakwa ya kanuni za fedha.

“Kwa mfano kulikuwa na malipo yaliyofikia Sh bilioni 3.5 ambazo zilifanywa bila kuidhinishwa na Katibu Mkuu na Mweka Hazina wa CWT kati ya kipindi cha 2011 na 2016.

“Ukaguzi wa CWT ulifanyika kwa maombi maalumu kwa kuwa si sehemu ya mashirika ya umma na baada ya ukaguzi huo ilibainika taasisi hiyo kutoendeshwa sawa sawa,” alisema.

 

MAMLAKA SERIKALI ZA MITAA

Alisema ripoti yao imebaini jumla ya serikali za mitaa 146 hazikupata Sh bilioni 582 ambazo ni sawa na asilimia 15 ya bajeti yote ya Serikali ya Mitaa.

“Tulikuwa tunaomba kwamba tukipanga bajeti basi itolewe ili serikali za mitaa zifanye kazi zake kama zilivyopangwa.

“Eneo la pili ni fedha za maendeleo hazitolewi na zinafika serikali za mitaa 167 ambazo hazikupokea Sh bilioni 532 sawa na asilimia 51, hizo fedha ni nyingi zisipokwenda, serikali za mitaa zitashindwa kuekeleza malengo yake.

“Kingine tulichobaini, mapato ya ndani hazikusanyi mapato yake yenyewe, aidha wao wenyewe au kupitia mawakala, na tumeona hili katika serikali za mitaa 140 ambazo zilishindwa kukusanya Sh bilioni 116 sawa na asilimia 22 ya mapato yake.

“Zaidi ya hayo, mawakala kutokuwasilisha Sh bilioni  3.5 ya fedha ambazo wamekusanya, lakini hawakuwasilisha, nadhani ni usimamizi mbovu wa halmashauri.

“Kuna vitabu 379 vya mapato ambavyo hatukuviona, hivyo kitabu cha mapato kisipokuja kwetu hatujui kimetumikaje, hatuwezi kujua kiasi gani kilichopotea na ni vitabu hivyo ni vingi sana.

“Pia tumebaini udhaifu katika rasilimali watu na madai ya mishahara ya Sh bilioni 10 katika mamlaka za serikali za mitaa 19 hayakulipwa. Hilo tumeona ni tatizo,” alisema.

 

VYAMA SABA HATI CHAFU 

Profesa Assad alitaja vyama vya siasa ambavyo vimepata hati chafu kuwa ni pamoja na Sauti ya Umma, National League For Democracy (NLD), Tanzania Democratic Alliance (TADEA), Alliance for Democratic Change (ADC), Tanzania Labour Party (TLP) na Demokrasia Makini.

Alisema sheria inawataka kukagua vyama vya siasa na kwamba haijalishi kama havipati ruzuku.

 

JPM AWASIMAMISHA WAKURUGENZI

Katika hafla hiyo, Rais Magufuli alimwagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo, kuwasimamisha wakurugenzi wa Halmashauri ya Kigoma Ujiji na Pangani kutokana na kupata hati chafu.

“Halmashari mbili zina hati chafu, Kigoma Ujiji na Pangani. Nafikiri saa zingine tuchukue hatua, Waziri wa Tamisemi wakurugenzi wa hizo halmashauri wasimamishwe leo (jana), inawezekana si vizuri, lakini tuchukue hatua na CAG ni mtu wa Mungu, hawezi kusingizia mtu,” alisema Rais Magufuli.

Hata hivyo, taarifa iliyotolewa na Ikulu jana jioni, ilionyesha kufuatia ripoti hiyo, Rais Magufuli amemwagiza Waziri wa Tamisemi, Jafo, kuwasimamisha kazi wakurugenzi wa halmashauri tatu za Kigoma-Ujiji, Kigoma Vijijini na Pangani kutokana na halmashauri zao kupata hati chafu na ameahidi Serikali itafanyia kazi ripoti hiyo ya CAG na kuchukua hatua stahiki.

Akizungumzia kuhusu kesi za rufaa za kodi ya Sh trilioni 4.4 ambazo hadi sasa hazijafanyiwa uamuzi na mahakama, Rais Magufuli alimwagiza Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, kujadiliana na Jaji Mkuu ili ziamuliwe haraka.

“Umejaribu kueleza jinsi kesi zilizoko mahakamani za Sh trilioni 4.4 ambazo hazijawa ‘solved’ ambapo Serikali kwa ujumla bado tunahitaji fedha, tunashukuru sana kwa ushauri wako,” alisema Rais Magufuli.

Rais Magufuli alisema Serikali itatumia ushauri uliotolewa kwenye ripoti hiyo na kuwa matokeo yake yataonekana mapema.

 

JAFO ATOA TAARIFA

Jana jioni, Waziri Jafo alitoa taarifa kwa umma akisema amewasimamisha wakurugenzi watatu ambao halmashauri zao zimepata hati chafu.

Aliwataja kwa majina wakurugenzi hao ni pamoja na Judethadeus Mboya (Kigoma Ujiji) ambaye taarifa hiyo ilisema amestaafu.

Wengine ni Hanji Godigodi (Kigoma) na Sabas Chambasi (Pangani).

“Wakurugenzi hao ambao halmashauri zao zimepata hati chafu, nawasimamisha kazi kuanzia leo (jana) hadi hapo uchunguzi wa utendaji wao kazi utakapomalizika,” alisema Jafo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles