23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Ridhiwani akerwa migogoro isiyokwisha Chalinze

Na Mwandishi Wetu, Pwani

Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwani Kikwete, amesema anakerwa na migogoro isiyokwisha baina ya vijiji na vijiji kuhusu mipaka na ile ya wakulima na wafugaji ndani ya jimbo hilo.

Akizungumza leo Desemba 15, katika mkutano wake uliofanyika Kata ya Kimange kushukuru na kupokea kero na maoni ya wananchi uliofanyika Kijiji cha Pongwekiona na Kimange kwa nyakati tofauti, Ridhiwani, amesema migogoro hiyo inakwamisha juhudi za kuleta maendeleo jimboni humo.

Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwani Kikwete (katikati), akifafanua jambo katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Kimange jimboni Chalinze jana

Akijibu hoja iliyowasilishwa na wananchi, Ridhiwani, amewaagiza viongozi wa Serikali za Vijiji hivyo wasimamie sheria walizojiwekea ili kuondoa migongano isiyokwisha ikiwamo ya wakulima na wafugaji.

Ridhiwani ambaye kitaaluma ni mwanasheria, pia amewashauri wananchi na hasa Serikali za Vijiji hivyo juu ya umuhimu wa kufuata sheria ili kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji na pia wanapotaka kujadili migogoro na vijiji vingine.

Pia amewaomba wananchi waendelee kumuunga mkono Rais Dk. John Magufuli katika juhudi zake za kuwakomboa wananchi wanyonge katika vitendo vya ukandamizaji vinavyofanywa na wachache wenye tamaa hasa katika elimu, afya, ardhi na kusaidia kuwakomboa wananchi katika umasikini.

“Rais wetu Magufuli anawashukuru sana kwa kura nyingi na amewaahidi kuwatumikia wananchi wake. Kura mlizompa ni kielelezo cha imani kubwa tuliyonayo wana Chalinze kwake na Serikali yake. Rais ametuahidi mambo makubwa na kwa heshima hii ametuahidi hatotuacha.

“Tulichonacho sasa ni kujipanga vizuri kwa utekelezaji wa majukumu kama alivyotuelekeza. Hivyo sisi kama wasaidizi wake jukumu letu ni kufanya kazi naye kuhakikisha nia yake inatimia na kwa kuanza tuanze kujikagua sisi wenyewe kama tunafanya yale aliyoyaelekeza,” amesema Ridhiwani.

Katika ziara hiyo, kero za migogoro ya baina ya wafugaji na wakulima ziliibuka na ameagiza kuendelea kusimamia sheria ikiwamo za vijiji na zile za Serikali Kuu ili kuleta usawa baina ya pande zote mbili.

Mbali na kero hiyo, baadhi ya wananchi wa Pongwekiona walimuomba Ridhiwani kusimamia maboresho ya barabara inayotoka Kimange-Pongwekiona ili iweze kupitika wakati wote bila shida.

Wakitoa kero hizo, wananchi hao wamesema wanapata vikwazo pindi wanapoumwa ama mjamzito anapotakiwa kuwaishwa kupata huduma za afya katika Hospitali ya Wilaya Chalinze.

“Mbunge wetu chondechonde wananchi wako huku Pongwekiona tuna shida kubwa ya barabara hasa wakati wa masika, hii barabara haipitiki na nadhani mmejionea wakati mnakuja huku.” Amesema Saumu Hamisi ambaye ni mkazi wa Pongwekiona.

Kwa upande wake, Mwanawetu Salumu, amesema barabara hiyo imekuwa kero kubwa ikiwamo kushindwa kusafirisha bidhaa zao hoja iliyoungwa mkono na wananchi wote waliokuwapo katika mkutano huo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles