Na Mohamed Hamad, Kiteto
Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania, kimeanza kufuatilia miti 10, 000 iliyopandwa maeneo tofautitofauti wilayani Kiteto, Mkoa wa Manyara kwa ajili ya kufuatilia maendeleo yake.
Miti hiyo ni ile iliyopandwa kwenye maeneo ya Taasisi, Zahanati, Shule, Nyumba za ibaada kwa ajili ya matunda na kimvuli.
Akizungumzia katika ukaguzi wa miti hiyo, Meneja wa Mradi wa Usalama wa Chakula Kiteto, Haruni Mvungi amesema kwa sasa maendeleo ya miti hiyo ni mazuri akisisitiza ulinzi uongezeke zaidi ili isiliwe na mifugo.
Amesema miti hiyo imegharimu fedha nyingi zaidi ya Sh milioni 30,000 hivyo itakapokua italeta manufaa makubwa na endapo haitatunzwa na kufa italeta hasara.
Miti hiyo imepandwa kwenye maeneo yanayofikiwa na mradi huo ambayo ni vijiji vya Orpopong’i, Ndaleta, Njoro, Ndedo na Makame ambavyo vilipata idadi tofauti kulingana na maombi.
Mbali na ukaguzi wa miti hiyo pia viongozi hao wamefika kuona mashamba darasa yaliyopandwa nyasi pamoja na mahindi kata ya Makame ili kukabiliana na ukame akisema maendeleo yake ni mazuri.
Jumla la wanufaika 2,000 ambao ni wakulima na wafugaji kaya maskini walipatiwa msaada huo ambapo watu 1,000 walipewa mbegu za mahindi na 1,000 walipatiwa chakula cha mifugo majani na mashudu pamoja na mbegu za majani kwa ajili ya kulima.
Lengo la misaada hiyo ni kukabiliana na ukame ambapo mwaka 2020-2021 kwa mujibu wa mamlaka ya hali ya hewa TMA wilaya ya Kiteto imetajwa kuwa itakuwa na mvua chache ambazo zitakuwa chini ya wastani.
Baadhi ya wananchi wa maeneo hayo ya mradi akiwemo, Rasidi Juma wa Kijiji cha Ndaleta na Naitapaki Mbaiyoo wa Kijiji cha Makame wameeleza kuwa Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania kimekuwa msaada mkubwa katika maeneo yao.