30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

RC Rukwa aonya wanaotumia bandari bubu kuingiza corona

Na Mwandishi wetu-Rukwa

MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo amewataka viongozi wa vitongoji, vijiji na watendaji wa kata za Korongwe na Kabwe kuhakikisha wanawahamasisha wananchi kuwa mstari wa mbele katika kuilinda nchi na virusi vya corona kwa kuzuia uingiaji holela wa wageni wanaoweza kuuleta ugonjwa huo kutoka nchi za jirani.

Wangabo alisema hadi sasa Mkoa wa Rukwa umewaweka karantini watu 49 ambapo kati yao Watanzania ni 36 na wageni 13.

Alisema watu hao walipita katika bandari na mipaka rasmi ya mkoa huo huku akisema utaratibu wa kuwaweka watu karantini, hauangalii uraia wa mtu wala hadhi yake.

Aliwataka viongozi hao kuwaelimisha wananchi kuwakataa wageni wasiotumia mipaka na bandari rasmi kuingia nchini.

Alisema kuruhusu wageni hao kutailetea nchi maafa na hivyo kuwataka viongozi na wananchi kuacha matumizi ya bandari bubu zilizopo katika vijiji vya mwambao wa Ziwa Tanganyika.

“Watu wapite maeneo ambayo ni rasmi, waje hapa kwenye Bandari ya Kabwe, wapite hapo na taratibu nyingine za kiafya zitafanyika, lakini si kwenye bandari bubu huku.

“Ndani ya Wilaya ya Nkasi kuna bandari bubu 46, Nkasi peke yake na katika Kata ya Korongwe na Kabwe kuna bandari bubu 13, ndio maana nikasema viongozi ninyi wa kata mbili hizi mje hapa, ili muone umuhimu wa kuzuia watu wanaotumia bandari hizi bubu,” alisema Wangabo.

Kamanda wa Uhamiaji Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi Elizeus Mushongi, alitahadharisha matumizi mabaya ya madaraka ya viongozi hao ambao huwapokea wageni na kuwaruhusu kuingia nchini bila ya kufuata utaratibu wa Serikali.

Alisema matumizi ya bandari bubu ni haramu na hivyo atakayekamatwa anayahalalisha hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.

“Wageni kutoka nje ya nchi, iwe Kongo, Burundi, Zambia, mnawapokea kule na nyinyi ndio mnakuwa maafisa uhamiaji, mnakuwa maafisa forodha, kila kitu mnamaliza wenyewe kule, sasa kama mtampokea mtu anaumwa ule ugonjwa, ninyi ndio mtakaoanza kuupokea na mtaenda kuambukiza familia zenu.

“Niwaombe sana msipokee watu kutoka nje ya nchi kama hawajapita katika vituo vilivyoainishwa kisheria,” alisema Wangabo.

Diwani wa Viti Maalumu, Christina Simbakavu alisema kuna baadhi ya watu wenye ndugu zao nchi ya jirani ya DR Congo na huwa na kawaida ya kuingia katika vijiji hivyo nyakati za usiku bila kufuata taratibu.

 “Kuna boti zinazoingia usiku kama alivyotamka mjumbe wa Kijiji cha Kalila, zile boti zinaingia lakini wenyeji wenye ndugu zao kutoka nchi jirani ya Congo wanawapokea katika mazingira ambayo si rafiki sana na hawatoi taarifa,” alisema Simbakavu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles