Na JUDITH NYANGE – MWANZA
MKUU wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, amekasirishwa na kitendo cha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kufunga shule za msingi 11 kwa kukosa vyoo.
Pia ametaka kukutana na viongozi wote wa Ukerewe na kamati inayowahusisha wakuu wa idara wa wilaya hiyo waweze kumweleza ni sababu zipi zilizowafanya kufunga shule zote hizo.
Hayo yalibainika jana kwenye kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa huo (RCC) wakati Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe, Frank Bahati, alipowasilisha hoja ya maombi ya bajeti maalumu.
Akiwasilisha hoja ya maombi maalumu ya wilaya hiyo, Bahati alisema uongozi ulilazimika kuzifunga shule hizo kutokana na ukosefu wa vyoo.
Alisema katika bajeti hiyo ya maombi maalumu wilaya inaomba Sh bilioni 8.1 kwa ajili ya ujenzi wa vyoo katika shule hizo zilizofungwa ziweze kujengewa vyoo kabla ya kufunguliwa.
RC Mongella alishangazwa na kauli hiyo kwa kumkatisha Bahati na kumhoji ni wapi walipowahamishia wanafunzi waliokuwa wakisoma katika shule hizo 11 za msingi na nani aliyempa kibali cha kufunga shule hizo.
Alijibu swali hilo, Bahati alisema wanafunzi hao kwa wapo nyumbani tangu shule hizo zifungwe.
"Sheria ya elimu inasema hakuna mtu yeyote mwenye mamlaka ya kufunga shule isipokuwa Kamishna wa Elimu pekee.
“Hata Rais au waziri wa elimu hawezi kufanya hivyo lazima ashauriane na kamishna kama kuna umuhimu wa kufanya hivyo.
"Nyie mmefunga hizo shule kwa kibali au ruhusa ya nani DC Ukerewe una hizi taarifa? Maana mimi mwenyewe ninayetakiwa kumshauri kamishna kufanya hivyo ndiyo kwanza naliskia hapa, " alisema.
Katika kikao hicho wakurugenzi wa halmashauri zote za mkoa wa Mwanza waliwasilisha maombi ya bajeti maalumu za maeneo yao.
Suala hilo lilimshangaza Mongella na kulazimika kutafuta uzoefu kwa kuwahoji wakurugenzi wazoefu waliohudhuria kikao hicho.
Wakurugenzi hao walisema kwa uzoefu walio nao maombi ya bajeti maalumu hayatakiwi kuzidi Sh milioni 700 au Sh bilioni 1. 5.
Walisema bajeti iliyowahi kuzidi kiwango hicho ni ile iliyotolewa kwa Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa na hiyo ilitokana na halmashauri hiyo kuwa mpya.
Mongella aliagiza hoja hiyo ifutwe hadi atakapokutana na wakurugenzi hao na kuijadili kwa vile kiasi cha fedha kinachoombwa na halmashauri zote kinazidi makusanyo ya ndani ya mkoa mzima.