25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Samia asimikwa na machifu kuwa Chifu Mkuu, apewa jina la hangaya

Na Clara Matimo, Mwanza

Umoja wa Machifu Tanzania(UMT) leo umemsimika Rais Samia Suluhu Hassan kuwa chifu  Mkuu wa Tanzania na wamempa jina la hangaya lenye maana ya nyota angavu.

Zoezi hilo la kumsimika kuwa Chifu Mkuu wa Tanzania limefanyika katika uwanja wa msalaba mwekundu(ngomeni) uliopo wilaya ya Magu Mkoani Mwanza baada ya kumaliza kuhutubia  machifu na  mamia ya wananchi waliofurika uwanjani hapo kwenye kilele cha tamasha la utamaduni mila na desturi zetu lililoandaliwa na UMT.

Akizungumza wakati akimsimika uchifu Rais Samia Suhulu Hassan, Mwenyekiti wa Umoja wa Watemi wa Usukuma, Itale Charles, amesema nyota angavuni nyota ya asubuhi  ambayo inangaa alfajiri kabla ya jogoo kuwika  kwa mara ya pili inayohimiza watu kuamka na kwenda kuwajibika.

 “Ni  nyota inavyoashiria matumaini, kama ambavyo wewe  rais wetu umekuwa na matumaini makubwa kwa watanzania na watanzania tunamatumaini makubwa na wewe, tumekupa  jina hili kwa kutambua mchango wako katika kusimamia na kuthamini utu wa wanyonge na utamaduni wetu,”amesema Chifu Itale.

UMT wamemkabidhi Chifu Mkuu wa Tanzania, Rais Samia vitu mbalimbali

Nguo nyeusi ambayo ni alama ya mawingu meusi yanayoleta mvua watu wanalima na  kupata chakula hivyo wamemtaka awe baraka kwa watanzania,  nguo nyekundu, ngao na mkuki   vinawakilisha alama ya ulinzi avitumie kama silaha  kulinda nchi yake pamoja na ngozi ya chui kwa kuwa ni  mnyama mpole  lakini ni mlinzi hodari kwa watoto wake wamemtaka awe mpole kwa watanzania wote lakini  mwangalifu kwa wanaotaka kuwadhuru wananchi wake au nchi yao.

Pia wamemvisha ushanga uliotengenezwa kwa ganda la yai la mbuni maana ni ndege pekee aliyemwangalifu sana kwa vifaranga vyake anaweza hata kupigana na wanyama wakali kama fisi   ili kuwalinda watoto wake wasiweze kupata madhara na yeye watanzania ndiyo vifaranga vyake wamemuomba awalinde na kuwalea.

Usinga ukiwakilisha watanzania kama ambavyo mtu hawezi  kuhesabu singa kutokana na wingi wake hivyo naye  ana watu awatumie kuleta maendeleo ya nchi akawalinde,  kiti cha kiutawala  chenye  mguu mmoja kikimaanisha  yeye ndiye chifu mkuu hakuna mwingine akitumie kukaa na kuwasikiliza  wananchi wake  wazungumze na kupata muafaka wa mambo mbalimbali watakayoyajadili.

Chifu Mkuu wa Tanzania atoa neno baada ya kusimikwa

Akizungumza baada ya zoezi la kusimikwa kuwa Chifu Mkuu wa Tanzania kukamilika, Rais Samia  ameahidi kushirikiana na machifu wote nchini kuendeleza tamaduni  mila na desturi  za watanzania kwa faida ya vizazi vijavyo.

“Nawashukuru sana UMT kwa kunipa jina hili zuri namuomba Mungu anisaidie nising’are peke yangu ning’are na wananchi wangu pamoja na nchi yangu naahidi kushirikiana nanyi katika kuhakikisha tamaduni zetu tunazilinda,”amesema.

Awali Mratibu wa Tamasha hilo, Chifu Aron Mikomangwa Nyamilonda wa III akisoma hotuba ya UMT mbele ya Rais Samia, ameiomba serikali kuwatambua rasmi na kuwapa usajili waungane na serikali kulinda utamaduni wa nchi,  eneo la ardhi makao makuu  Dodoma kwa ajili ya kuweka ofisi na miradi itakayowezesha umoja huo kujiendesha kiuchumi.

“Pamoja na maombi hayo mheshimiwa rais  tunakabiliwa na changamoto mbalimbli  ikiwemo  kupoteza umiliki wa majengo yetu,  upatikanaji wa nyara za serikali kwa ajili ya kuzitumia  kwenye shughuli zetu za kila siku, ubovu wa miundo mbinu kwenye vituo vya makumbusho na kuvamiwa kwa maeneo ya himaya za jadi.

“Vituo vingi vya makumbusho vinahitaji kuboreshwa kufikia kiwango cha kimataifa hata vile visivyopokea ruzuku kutoka serikalini mfano miundombinu ya  majengo  katika  kituo cha makumbusho cha  bujora ni mibovu hicho ni  kituo pekee duniani kinachoonyesha  utamaduni halisi wa kabila la wasukuma na watanzania.

“Tunaomba ukiboresha  kituo hicho kitakuwa ni kituo bora kitakachouinua utamaduni wetu, tunaomba uwanja huu  wa ngomeni  ambapo tamasha hili linafanyika urudi kwa waasisi ambao ni wananchi wa eneo hili na  machifu,”amesema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles