33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

RAIS SAHIHI WA TFF AZINGATIE  HAYA…….

Na ADAM MKWEPU-DAR ES SALAAM


UCHAGUZI Mkuu wa Shirikisho la soka Tanzania (TFF), unaotarajiwa kufanyika Agosti 12 mwaka huu huenda ukawa na matokeo tofauti na inavyotarajiwa kutokana  na wadau wengi  kutaka mabadiliko ya kiuongozi na utendaji katika shirikisho hilo.

Wanaotarajiwa kufanya mabadiliko hayo ni wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, ambao watapiga kura kuchagua viongozi akiwamo rais mpya wa shirikisho hilo.

Huu ni uchaguzi ambao kila mwanafamilia wa mchezo wa soka nchini anatamani matokeo yake, baada ya kupiga kura. Miongoni mwa wapiga kura hao, wapo wanaotamani kuendelea na uongozi ule ule wa rais wa TFF, Jamali Malinzi wakati wengine wakitaka mabadiliko ya kiungozi ili kupisha mawazo mapya wakiamini yatasaidia maendeleo ya mchezo wa soka.

Lakini uchaguzi  huo umekuwa na wagombea wenye sifa tofauti za kiuongozi na kutokana na suala hilo, kuna kila sababu kwa watakaopata nafasi ya kupiga kura kuchagua ambaye atakuwa na sifa zenye kustahili kuliongoza shirikisho hilo.

Licha ya wapiga kura kutofautiana kimtazamo katika hili, wanatakiwa kufanya uamuzi utakaolisaidia shirikisho hilo kupata mtu sahihi wa kuliendesha.

Kwa muda mrefu wadau na wapenzi wa soka nchini wamekuwa wakilalamika kuhusu mapungufu kadhaa ndani ya shirikisho hilo, likiwamo suala la uweledi, mapungufu ya usimamizi wa sheria katika kutoa haki kwa wanachama pamoja na upungufu wa ufahamu wa mchezo wenyewe bila kusahahu hofu ya Mungu katika kuliongoza shirikisho hilo.

Hizo ni moja ya sifa za rais na viongozi wanaotakiwa kusaidia kufanikisha safari ya Watanzania wapenda soka.

Mchezo wa soka nchini umekosa watu wa uhakika ambao kimsingi wanaweza kusimama kidete katika kuliokoa soka la taifa hili.

Kumekuwa na vipindi kadhaa vya kiuongozi ndani ya TFF, lakini wanaonekana wakishughulika zaidi kutatua matatizo, badala ya kuandaa mipango mipya ya kulitoa soka lililopo na kulipeleka sehemu inayotakiwa kwa ustawi wake.

Ndani ya TFF kwa vipindi tofauti kumekuwa na hutofauti wa mitazamo baina ya viongozi wakuu, wengine wakipinga mipango na mikakati inayotumika katika kuendesha shirikisho hilo.

Mfano mzuri, ni suala la uchaguzi wa mikoa iliyomalizika hivi karibuni, pamoja na malalamiko kila kukicha kutoka kwa wanachama wa shirikisho hilo, huku wengine wakionekana kutotendewa haki.

Ni jambo la aibu na kutokubalika kwa TFF kuendeshwa kama genge la watu wachache, wenye mitazamo yenye maslahi binafsi na kuliacha soka likiteketea.

Kutokana na sababu hizo, kwa haraka haraka zinaweza kuchangia mabadiliko makubwa ya kiuongozi katika uchaguzi huo, ambao umekuwa na hamasa kutoka na wadau wanaotaka mabadiliko.

Kwa ujumla litakuwa jambo la busara kama watakaopiga kura wakizingatia sifa sahihi za viongozi, wanaotakiwa na wanafamilia ya wapenda soka.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles