31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Magufuli aendelea Kujaza nafasi wazi

Na mwandishi wetu- Dar es Salaam

RAIS Dk. John Magufuli amefanya uteuzi wa Mkuu wa Wilaya mmoja na wakurugenzi wa halmashauri watano, iikiwa ni siku moja tangu aapishe wakuu wa mikoa wawili, Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Katibu Tawala wa Mkoa mmoja na kuhushudia wakuu wa wilaya tisa wakiapishwa na wakuu wa mikoa Ikulu, Chamwino mkoani Dodoma.

Juzi Rais Magufuli alimuapisha Kamishna wa Polisi Thobias Andengenye kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dk. Philemon Sengati kuwa Mkuu wa Mkoa Tabora, James Kaji kuwa Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya na Mariam Perla Mmbaga kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu.

Jana Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Gerson Msigwa, alitoa taarifa kwa umma ikisema Rais Magufuli amemteua Lauteri Kanoni kuwa Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe Mkoani Njombe. 

Ilisema kabla ya uteuzi huo, Kanoni alikuwa Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia Serikali za Mitaa katika Mkoa wa Songwe na anachukua nafasi ya Ally Kasinge.

Ilisema pia Rais Magufuli amemteua Bashir Mhoja kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa.

“Kabla ya uteuzi huo, Mhoja alikuwa Mwanasheria wa Halmashauri ya Mji wa Geita mkoani Geita na anachukua nafasi ya Robert Masunya,” ilisema.

Ilisema pia Rais Magufuli amemteua Ramadhan Possi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze mkoani Pwani na kwamba kabla ya uteuzi huo,  Possi alikuwa Ofisa Mipango katika Jiji la Tanga  ambapo anachukua nafasi ya  Amina Kiwanuka ambaye amestaafu.

Taarifa hiyo pia ilieleza kuwa Rais Magufuli amemteua Baraka Zikatimu kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Urambo Mkoani Tabora.

Ilisema kabla ya uteuzi huo, Zikatimu alikuwa Ofisa Mipango katika Halmashauri ya Wilaya ya Bumbuli Mkoani Tanga na anachukua nafasi ya Margareth Nakainga ambaye amestaafu.

“Rais Magufuli amemteua John John Nchimbi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Babati Mkoani Manyara. Kabla ya uteuzi huo, Nchimbi alikuwa Ofisa Rasilimali Watu katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro mkoani Morogoro,” alisema.

Ilisema pia Rais Magufuli amemteua Emmanuel Johnson kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga na kwamba kabla ya uteuzi huo, Johnson alikuwa Ofisa Elimu wa Wilaya ya Kwimba Mkoani Mwanza.

Katika hatua nyingine, juzi jioni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Mkuchika, alifanya uteuzi wa Makatibu tawala wa wilaya sita.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyosainiwa na Katibu Mkuu Utumishi, Dk Laurean Ndumbaro, walioteuliwa ni Hassan Ngoma kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Singida Mkoani Singida ambaye anachukua nafasi ya Wilson Shimo ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Nyang’wale mkoani Geita.

Wengine ni Kamana Simba aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Longido, mkoani Arusha ambaye anachukua nafasi ya Toba Nguvila ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni mkoani Tanga.

Pia Faraja Msigwa ameteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha ambaye anachukua nafasi ya Abbas Kayanda ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Karatu.

Wengine ni Bahati Joram aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Malinyi, mkoani Morogoro akichukua nafasi ya Lameck Lusesa.

Pia Salum Mtelela aliteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Bunda, mkoani Mara kuchukua nafasi ya Jonas Nyehoja aliyestaafu.

Augustino Chazua ameteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro akichukua nafasi ya Robert Selasela.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles