27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Rais amkingia kifua Valverde

BARCELONA, HISPANIA

BAADA ya timu ya Barcelona kukosa ubingwa wa Kombe la Copa del Rey huku ikikubali kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Valencia juzi, rais wa timu hiyo, Josep Maria Bartomeu, amedai kocha wao, Ernesto Valverde hana kosa lolote.

Mbali na Barcelona kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Hispania, lakini kocha huyo amekuwa na wakati mgumu kutoka kwa mashabiki ambao wamekuwa wakishinikiza afukuzwe kutokana na kiwango kibovu kinachooneshwa na timu hiyo.

Mashabiki wanadai kuwa, kocha huyo amekuja kuua falsafa ya timu, ikiwa baada ya kushindwa kufanya vizuri kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa msimu uliopita pamoja na msimu huu kwa kuondolewa na Liverpool katika hatua ya nusu fainali kwa kichapo cha mabao 4-0 wiki kadhaa zilizopita.

Lakini baada ya mchezo huo wa juzi kumalizika, rais aliweka wazi kuwa uongozi hauna mpango wowote wa kumfukuza kocha huyo kutokana na matokeo waliyoyapata.

“Kila mara nimekuwa nikisema kuwa kocha huyo bado ana mkataba hadi msimu ujao, sidhani kama anatuhumiwa kwa lolote, wachezaji wetu walipata nafasi nyingi katika mchezo huo lakini walishindwa kuzitumia nafasi hizo na kufunga mabao.

“Lakini tuliweza kupata bao moja ila wapinzani wetu walituzidi bao moja na kuwa mabingwa wa kombe hilo, naweza kusema huu haukuwa msimu wetu wa mafanikio makubwa, lakini siwezi kusema kuwa ni msimu wetu mbaya kwa kuwa tumeweza kufika katika fainali hii pamoja na nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Mwisho wa siku tumepoteza nafasi mbili ila tumemaliza nafasi ya pili kwenye Copa del Rey,” alisema rais huyo.

Kwa upande wake, kocha Valverde alisema ni nafasi ya kipekee kwake kuweza kufika fainali kwenye kombe hilo hata kama ameshindwa kufanya vizuri.

“Siku zote makocha tumekuwa tukitaka kufanya vizuri, kama ningepewa nafasi ya kuchagua kutolewa kwenye hatua ya fainali au robo fainali na 16 bora, ningesema nitolewe fainali, tulikuwa na lengo la kutwaa ubingwa lakini hatujafanikiwa, furaha yangu ni kuona tumefika fainali,” alisema kocha huyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles