23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Profesa Kilian: Ajenda ya rushwa ilirudisha umaarufu wa CCM

FARAJA MASINDE-DAR ES SALAAM

NAIBU Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Tafiti, Profesa Bernadeta Kilian, amesema Chama Cha Mapinduzi (CCM) kisingeweza kurudisha umaarufu wake kama kisingechukua suala la rushwa kama moja ya ajenda zake kuu katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Profesa Bernadeta alitoa kauli hiyo jana katika kongamano la kujadili nafasi ya taasisi za elimu ya juu katika mapambano dhidi ya rushwa nchini lililofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Alisema hadi kufikia mwaka 2015 CCM ilipoteza umaarufu huku vilio dhidi ya vitendo vya rushwa  vikiongezeka siku hadi siku.

Profesa Bernadeta alisema  katika wa mfumo wa chama kimoja cha siasa, vitendo vya rushwa vilikuwa chini na kwamba upatikanaji wa taarifa ulikuwa mgumu kutokana na uchache wa vyombo vya habari.

“Ujio wa vyama vingi vya siasa na uhuru wa vyombo vya habari kipindi ndiyo vitendo vya rushwa vilikuwa vingi likiwamo suala la Escrow.

“Awamu zote zimekuwa zikionesha juhudi za kupambana na rushwa, hata hivyo kumekuwapo na mkwamo unaokwamisha juhudi hizo, hasa kwa  kushindwa kuwafikisha baadhi ya watuhumiwa mahakamani. Ili kuzuia mkwamo huo ni lazima kuwa na utashi wa kisiasa na kujenga utamaduni wa uwajibikaji kuanzia chini,” alisema Profesa Bernadeta.

Alisema kuna uhusiano mkubwa wa kiuchumi, kijamii na kisiasa katika mapambano dhidi ya rushwa ambayo hutegemea zaidi utashi wa kisiasa  wa viongozi  wakuu wa nchi.

Makamu wa Rais wa Serikali  ya Wanafunzi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Daruso), Jackline  Ndombele,  alisema vijana wengi wanajihusisha na rushwa hususani ya ngono kutokana na kutowajibika na kuamini kuwa kila kitu kitakwenda  sawa baada ya kumaliza masomo.

Jackline alisema licha  ya wasichana wengi kukabiliwa na tatizo la rushwa ya ngono,  ufuatiliaji wake umekuwa mgumu kutokana na kukosekana ushahidi jambo linaloonesha kuwa wasichana wengi hawafahamu jinsi ya kupata vielelezo.

“Niwatake vijana wenzangu hasa wa kike kuhakikisha tunapambana na vitendo vya rushwa na kutambua kuwa kwa nafasi yetu tukilichukulia jambo hili kama letu tutafanikiwa kuliko kutumia muda mwingi kujadili masuala yasiyo na tija katika  mitandao ya kijamii,” alisema Jackline.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia  na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mhandisi Kibeshi Kiyabo, alisema taasisi hiyo itafanya utafiti wa kitaifa wa kupambana  na rushwa ya ngono.

“Tunakubalina kwamba rushwa ya ngono ipo katika vyuo vikuu na sehemu nyingine nyingi lakini tunachokiona hapa sisi kama taasisi katika sheria namba 11 ya mwaka 2007 kifungu cha 25, rushwa ya ngono ni kosa la jinai wananchi wanatakiwa kufahamu hivyo.

“Hivyo unapoombwa rushwa ya ngono ujue anayefanya hivyo anaenda kinyume na sheria, hivyo Takukuru tupo tayari kwa ajili ya kulifanyia kazi na hata ambao wamekuwa wakifika kwetu tumekuwa wakiweka mitego na kuwakamata na hatua za kisheria zikichukua mkondo wake.

“Tayari tumefungua madawati kila ofisi ambayo ni maalum kwa ajili ya kuzungumzia rushwa ya ngono, tumefanyia hivi kwa sababu rushwa hii ni nyeti zaidi, wananchi waje Takukuru wavunje ukimya.

“Sheria ya mwaka 2007 inazuia mtu yoyote kunyanyasa mwananchi ambaye ametoa taarifa ya rushwa, hivyo ikabainika mtu aliyeoa taarifa ananyanyasika basi anachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria,” alisema.

Upande wake Mwakilishi wa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania  (TRA), Sospeter  Makubi, alisema rushwa na ukwepaji kodi ni moja ya changamoto  zinazoikabili mamlaka hiyo.

Alisema tafiti za Benki ya Dunia (WB) za hivi karibu ni zinaonesha nchi zenye viwango vikubwa vya rushwa hupoteza asilimia nne kutokana na rushwa huku.

Alivitaja baadhi ya vichocheo vya rushwa katika mamlaka hiyo kuwa ni pamoja na ukadiriaji viwango vya kodi, ukaguzi wa kodi, uondoaji wa mizigo ya forodha,  usajili wa magari pamoja na usimamizi wa mizigo inayosafirishwa kkwenda nchi mbalimbali kupitia nchini.

“Rushwa huchangia kwa kiasi kikubwa makusanyo ya kodi kushuka, hata kuongezeka kwa mikopo ya elimu ya ni kwa sababu makusanyo ya kodi yameongezeka, rushwa ikishamiri mikopo itapungua kwa sababu makusanyo ya tasks,” alisema Makubi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles