22.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Prof. Shemdoe Awaonya matapeli kuhusu ajira 6,000 za walimu

Veronica Simba na Atley Kuni

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, ametoa onyo kwa watu wanaowatapeli wananchi sehemu mbalimbali kwamba wanahusika kwa namna moja ama nyingine katika zoezi la kuajiri walimu 6,000 ili kujaza nafasi zilizoachwa wazi, kama ilivyoagizwa na Rais Samia Suluhu Hassan hivi karibuni.

Ametoa onyo hilo Aprili 23, 2021 mbele ya waandishi wa habari wakati wa ziara yake ya kwanza Makao Makuu ya Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) Dodoma, iliyolenga kujionea utekelezaji wa majukumu yao pamoja na kuzungumza na watumishi.

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe (katikati), akizungumza na Wajumbe wa Menejimenti ya Tume ya Utumishi wa Walimu – TSC (hawapo pichani), alipotembelea Taasisi hiyo jijini Dodoma Aprili 23, 2021 kujionea utekelezaji wa majukumu. Kushoto kwake ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, anayehusika na masuala ya Elimu, Gerald Mweli na kulia kwake ni Katibu wa TSC Mwl. Paulina Nkwama.

Prof. Shemdoe amewataka watumishi wa umma kuepuka kujihusisha na utapeli huo kwani wakibainika watachukuliwa hatua kali za kinidhamu na kisheria ikiwemo kufukuzwa kazi. Aidha, kuhusu vishoka wanaojihusisha na utapeli huo, Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa TAMISEMI itapambana nao vikali.

“Mtumishi atakayebainika kujiingiza kwenye suala hili la utapeli anaweza kupoteza kazi. Kwa wale vishoka ambao wameamua kujichukulia fedha za watanzania wenzetu wakiwahadaa kuwa watawatafutia ajira, tutapambana nao vikali na tutahakikisha sheria inachukua mkondo wake,”

Kufuatia hali hiyo, Prof Shemdoe amebainisha kuwa ajira husika zitatolewa kwa kuzingatia vigezo vitakavyoainishwa katika tangazo litakalotolewa na Ofisi yake, na kwamba hakutakuwa na upendeleo wa aina yoyote.

“Hakuna mtu atakayependelewa na hatutaangalia nani katoka wapi. Hizi ni ajira za watanzania wote, hivyo tutaangalia vigezo ambavyo tutaviainisha katika tangazo ambalo tutalitoa kwa wananchi na siyo vinginevyo,” amesisitiza.

Aidha, amemwagiza Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI, anayehusika na masuala ya Elimu, Gerald Mweli pamoja na Katibu wa TSC, Mwl Paulina Nkwama kukaa pamoja na kuunda timu itakayoshughulikia ajira hizo, huku akisisitiza kuwa timu hiyo iundwe na watu wenye hofu ya Mungu ili watende haki.

Amesema Ofisi yake itaendelea kuomba nafasi zaidi za ajira kwani inatambua kuwa wapo vijana wengi waliohitimu nab ado hawapata ajira.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu ameipongeza TSC kwa kazi nzuri inayofanya hususani katika kusimamia maadili kwa walimu walioko katika utumishi wa umma. Amewataka watendaji wa Taasisi hiyo kuendelea kutimiza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu hasa wakati wa kufanya maamuzi katika mashauri ya walimu yanayofikishwa kwao.

“Serikali imewapa dhamana na imani kubwa kwenu katika kusimamia maadili ya walimu. Nawaomba muendelee kufanya kazi hiyo kwa imani ileile ambayo mmepewa.”

Prof Shemdoe amempongeza Katibu wa TSC, Mwl Paulina Nkwama kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Rais Samia kushika wadhifa huo. Amewataka watumishi wote kumpa ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Katibu Mkuu Mweli, alimweleza Katibu Mkuu kuwa TSC imekuwa ikifanya kazi nzuri ambapo alibainisha kuwa tangu ashike nafasi hiyo, Tume imetekeleza kazi walizokubaliana kwa asilimia 90.

Kwa upande wake, akizungumza kwa niaba ya watumishi wote wa TSC, Katibu wa Tume Mwl Nkwama alisema kuwa wamefarijika sana kupata heshima ya kuwa miongoni mwa taasisi za mwanzo zilizo chini ya TAMISEMI, kutembelewa na Katibu Mkuu ili kujionea utendaji wao.

“Tumefarijika sana na ujio wako hasa kwa kuzingatia kuwa ni takriban majuma mawili tu tangu ulipoapishwa na Mhe. Rais kushika wadhifa wa Katibu Mkuu TAMISEMI. Kwa kuthamini, mchango wa kada ya walimu, umeona ziara yako ya kwanza ujielekeze kwenye Ofisi ya Tume ambayo ndiyo yenye kushughulikia masuala mbalimbali ya walimu. Tunaskushukuru sana,” amesema.

Tume ya Utumishi wa Walimu ndiyo Mamlaka ya Ajira na Nidhamu kwa walimu walioko katika utumishi wa umma Tanzania Bara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles