Na AVELINE KITOMARY-DAR ES SALAAM
MKURUGENZI wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Prof Mohamed Janabi, amesema sababu ya watu wanaofanya mazoezi kufariki ghafla ni pamoja na kutokupima afya zao kabla ya kufanya mazoezi ili kubaini aina ya mazoezi wanayotakiwa kufanya.
Akizungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalum, Prof Janabi ambaye ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo, alisema kwa kawaida mtu anaweza kuonekana hana tatizo lolote lakini kuna matatizo ambayo yanasubiri ufanye mazoezi kuliko uwezo wa moyo ndipo yaamke.
“Mazoezi ni kitu kizuri lakini asilimia kubwa ya watu wanafanya mazoezi bila kujua wanahitaji kufanya mazoezi ya aina gani, hii ni hatari ndiyo maana utakuta wengine wanapata matatzio ya ghafla.
“Shida ya moyo inatokea pale mtu anapokuwa na matundu moyoni, inasubiri siku utakapofanya kitu chenye nguvu zaidi kuliko uwezo wako, kuna watu moyo wao unamisuli mikubwa, hao ni kwamba njia inakuwa blocked na wengine wanakuwa na matundu kwenye moyo, watu kama hao wakifanya mazoezi magumu wanaweza wakapata madhara,”alisema Prof Janabi.
Aidha Prof Janabi aliwashauri watu wanapoenda kufanya mazoezi wapime kwanza afya zao ili waweze kuepukana na vifo vya ghafla.
“Ushauri wetu mkubwa kama madaktari kabla hujaenda kwenye gym, au kufanya mazoezi mengine makubwa kwanza upime afya yako kwasababu tunasikia wachezaji wanaanguka, wengine ni wanariadha awanaanguka wanafariki kwasababu hawajui wanatatizo gani.
“Mtu anaweza kupata tatizo la moyo au lingine, nakupa tu mfano timu yetu ya Taifa iliyokwenda AFCON (Kombe la Mataifa ya Afrika) walileta timu nzima ili kupima afya, wachezaji wawili walikutwa na matatizo makubwa kwahiyo wakaondolewa kwenye timu, hii imeweza kuokoa maisha yao maana unaweza kuanguka ghafla ukaambiwa eti umerushiwa jini mara, kafanyiwa hivi kumbe ni tatizo la moyo,”alifafanua Prof Janabi.
Licha ya kupima afya Prof Janabi aliwashauri watu kukutana na wataalam wa mazoezi ili waweze kuelezwa kuhusu aina ya mazoezi wanayotakiwa kufanya kulingana na afya au umri.
“Mazoezi wakati mwingine inategemea na umri, unaweza kuwa na miaka 70 halafu unaenda kukimbia mita 100, unajitafutia matatizo kwahiyo umri unategemea aina ya mazoezi, ni vyema ukapata mshauri akakwambia wewe kwa umri wako unatakiwa ufanye mazoezi ya aina hii,”alisema Prof Janabi.