23.9 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Posho usahihishaji mitihani yaondolewa

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia,  Profesa Joyce Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako.

NA MWANDISHI WETU – DAR ES SALAAM

POSHO za usahihishaji wa mtihani wa utamirifu (mock exams) na ile ya Taifa (National exams),sasa ni kizungumkuti baada ya Serikali kuamua kuzifuta.

Chanzo cha kuaminika kutokana serikalini, kimelieleza MTANZANIA kuwa  sababu iliyotolewa juu ya hatua hiyo, ni kwamba kusahihisha mitihani ni sehemu ya kazi ya walimu, hivyo hawahitaji kulipwa malipo yoyote ya ziada.

“Kabla Serikali haijafuta utaratibu huu, walimu waliokua wanaenda kusahihisha mitihani walikua wakipewa malazi (accomodation), chakula (meal) na posho ya Sh 500 kwa kila script moja anayosahihisha.

“ Kwa hiyo mwalimu akisahihisha scripts 100 kwa siku (wastani wa maswali 100) anapata Sh 50,000 na hiyo ni nje ya chakula na malazi ambavyo anahudumiwa na serikali,” kilisema.

Mara nyingi walimu walikua wakipiga kambi kwenye vyuo vya ualimu au shule kubwa za sekondari kwa ajili ya kusahihisha mitihani hiyo.

“Lakini kwa utaratibu mpya hakuna tena kupiga kambi kusahihisha mitihani ya Mock. Tawala za mikoa zimeagizwa kubuni utaratibu wa kusahihisha mitihani ambao utakuwa “zero cost”.

“Mkoa wa Geita, wameanza kutekeleza kwa kuagiza mitihani isahihishwe kwenye shule husika. Serikali imeamua kufuta posho katika mazingira ambayo walimu wamezuiwa kupanda madaraja hata kuongezewa mishahara,” kilieleza.

Chanzo hicho kilisisitiza “Ikumbukwe walimu ni miongoni mwa kada zisizo na posho wala marupurupu formal na walikua wakitegemea hizi za kusahihisha mitihani na kwenda kusimamia mitihani. Sasa zimefutwa rasmi, hii itafanya maisha yao kuendelea kuwa magumu maradufu, kuliko kipindi chochote katika historia.

MTANZANIA lilimtafuta Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi Stadi, Profesa Joyce Ndarichako kupata ufafanuzi juu ya suala hilo, lakini jitihada hizo ziligonga mwamba hadi tunakwenda mitamboni.

Na hata alipotafutwa Naibu wake, Injinia Stella Manyanya naye hakupatikana, ambapo mmoja wa maofisa habari wa Wizara hiyo alimshauri mwandishi kuwatafuta Baraza la Mitihani la Taifa kwani ndio wasimamizi wakuu wa mitihani hiyo.

Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa Necta, Dk. Charles Msonde alisema taarifa hizo hazina ukweli wowote.

“Necta ni wasimamizi wakuu wa mitihani ya kitaifa napenda umma utambue kwamba hakuna mabadiliko yoyote yaliyofanywa kuhusiana na utaratibu wa usahihishaji wa mitihani hiyo,” alisema.

Alisema taarifa yoyote isiyotolewa na Necta juu ya mitihani ya kitaifa si za kweli na kwamba zimelenga kupotosha umma.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles