29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

POLISI WAUA WENGINE WAWILI KIBITI

Mkuu wa Oparesheni Maalumu za Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Liberatus Sabas (Kushoto) na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Rufiji, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Onesmo Lyanga wakionyesha kwa Waandishi wa habari silaha mbili zilizopatikana baada ya mapambano katika msitu wa Ngomboroni Tarafa ya Ikwiriri ambapo katika tukio hilo waliuwawa wahalifu wawili wanaojihusisha na mauaji katika wilaya ya Mkuranga, Kibiti na Rufiji. (PICHA NA FRANK GEOFRAY-JESHI LA POLISI)

 

 

NA FRANK GEOFRAY-JESHI LA POLISI


JESHI la Polisi limefanikiwa kuwaua wahalifu wawili ambao ni miongoni mwa wanaoendesha mauaji katika Kanda Maalumu ya Polisi Rufiji kutokana na operesheni inayoendelea kwenye wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji mkoani Pwani.

Hatua hiyo imekuja baada ya wiki iliyopita, jeshi hilo kuua watu wengine wanne ambao wanadaiwa kuhusika na mauaji hayo ya viongozi wa vijiji na kisha kutokomea kusikojulikana.

Akizungumzia tukio hilo jana, Mkuu wa Operesheni Maalumu za Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Liberatus Sabas, alisema tukio hilo lilitokea juzi saa nne usiku katika msitu wa Ngomboroni, Kata ya Ikwiriri ambako askari walikuwa katika doria za ufuatiliaji wahalifu sugu wanaojihusisha na mauaji yanayoendelea.

Alisema askari wakiwa eneo hilo na mtuhumiwa mmoja muhimu anayeshiriki mauaji hayo, ambaye baada ya mahojiano alikubali kwenda kuwaonyesha mahali ambako ni maficho ya wenzake, kikundi cha watu watano walikurupuka kutoka kichakani na kuanza kukimbia, ndipo kwa tahadhari walianza mashambulizi na kufanikiwa kuwajeruhi wawili kwa risasi walipojaribu kutoroka.

Alisema kuwa majeruhi hao wawili akiwamo aliyawapeleka eneo hilo, walifariki dunia njiani wakati wakipelekwa hospitali kwa matibabu kutokana na kuvuja damu nyingi iliyosababishwa na majeraha ya risasi waliyoyapata.

Miili ya marehemu imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).

“Katika tukio hilo, tumefanikiwa kupata silaha mbili aina ya SMG, shotgun moja na risasi tisa za SMG zilizokuwa kwenye magazine,” alisema Sabas.

Mauaji ya viongozi wa vijiji na askari polisi ambayo yamekuwa yakiendelea kwa muda sasa katika maeneo hayo, yamesababisha zaidi ya watu 38 wakiwamo askari kuuawa bila hatia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles