27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Polisi Tanzania Inavyojihami kwa ligi kuu bara

Zainab Iddy

WAKAZI wa Mkoa wa Kilimanjaro, msimu ujao watapata fursa ya kuishuhudia tena Ligi Kuu Tanzania Bara(TPL), baada ya kuikosa kwa miaka 27.

Kwa kipindi chote hicho, mkoa huo haukuwa na timu Ligi Kuu, licha ya kuwa na timu nyingi zinazoshiriki Ligi Daraja   la Kwanza.

Mara ya mwisho Mkoa wa Kilimanjaro kuwa na timu Ligi Kuu ilikuwa mwaka 1992 ilipowakilishwa na timu ya Ushirika.

Mwaka huo huo ilishuka daraja na tangu wakati huo wakazi wake wamekuwa wakishuhudia timu za mikoa mingine.

Lakini kufuzu Ligi Kuu kwa timu ya Polisi Tanzania msimu ujao kumeleta faraja kubwa kwa wadau wa soka, ambao walikuwa na ana hamu kubwa ya kuona kipute cha TPL kikichezwa katika ardhi yao.

Polisi Tanzania itashiriki Ligi Kuu kwa mara ya kwanza msimu ujao utakaoanza kutimua vumbi Agosti 23 mwaka huu.

Namungo FC ya Ruangwa mkoani Lindi ni timu nyingine iliyofuzu Ligi Kuu sambamba na Polisi Tanzania.

Namungo pia itashiriki Ligi Kuu kwa kwa mara ya kwanza.

Nikirejea kwa Polisi Tanzania imepanga kutumia Uwanja wa Ushirika wa mjini Moshi kwa ajili ya michezo yake ya nyumbani, hatua inayoleta faraja kwa wananchi wa mkoa huo kujihakikishia  kuushuhudia mtangane wa TPL machoni mwao.

Polisi Tanzania ilipatikana baada ya Shirikisho la Soka Kimataifa (FIFA), kupitia kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kutoa utaratibu mpya unaozitaka taasisi na kampuni kuwa na timu moja katika Ligi Kuu, na ndipo Jeshi la Polisi Tanzania  lilipoamua kuunda timu moja itakayoliwakilisha.

SPOTI KIKI limezungumza na Kaimu Katibu Mkuu wa Polisi Tanzania,  Frank Geofrey,  ambaye anafunguka kuhusiana na maandalizi na mikakati yao ya msimu ujao.

Maandalizi

Frank anasema hatua ya kwanza waliyoifanya ni kuboresha benchi lao la ufundi, kwa kumpa mkataba kocha Selema Matola katika nafasi ya usaidizi pamoja na Ally Mtuli kutoka Zanzibar atakayekuwa kocha mkuu.

“Baada ya maboresho ya benchi la ufundi, ndipo harakati za usajili kwa wachezaji ulipoanza tuliwasajili Mohamed Yusuph, Kulwa Manzi, Green Poul, Willium Samson, Iddy Mobby, Wilium Lucian , Shaban Stambuli, Yassin Mustafa, Juma Ramadhan na Mohamed Mnanga.

“Wengine ni Mohamed Kassin, Kaleb Samwel, Pato Nganyani, Herinoco Kayombo, Bakari Majogoro, Hamad Mshamata, Hassan Nassoro, Bantu Admin, Dritram Nchimbi, Mohamed Mkopi, Erick Msagati, Sic Sabato, Edga Mfumakule, Marcel Kaheza, Patrick Madidi na Andrew Bulugu,”anaeleza.

Anasema mbali na usajili huo lakini pia kikosi chao kimecheza mechi za kirafiki kadhaa na mipango yao kabla ya msimu kuanza kiwe kimejipima na timu si chini ya saba.

Mikakati

Frank anasema jambo la kwanza ni kuleta ushindani katika Ligi Kuu Tanzania Bara, kwa kuhakikisha timu yao inasalia kwa misimu mingine.

“Uwezekano au kutowezekana kwa jambo hilo utajulikana mara baada ya mzunguko wa kwanza wa ligi kumalizika, ingawa lengo letu la pili ni kuweka historia ya kupanda daraja na kuchukua ubingwa wa ligi.

“Hili linawezekana kutokana na usajili tulioufanya, ambao umelenga wachezaji wa ndani zaidi ukizingatia hii ni taasisi inayojihusisha na masuala ya mambo ya ndani, lazima tutoe nafasi kubwa kwa wachezaji wetu wa ndani,”anasema.

Matola afunguka

Kocha Msaidizi wa Polisi Tanzania anasema hadi sasa kikosi chao kipo katika hali nzuri na hana shaka kitafanya vizuri katika Ligi Kuu.

“Binafsi naijua vizuri Ligi ya Tanzania kutokana na uzoefu nilioupata katika timu nilizopita, kulingana na usajili tuliofanya hatuna shaka tunaweza kuyafikia malengo kama si kumaliza ndani ya timu tano za juu katika msimamo  wa Ligi Kuu, basi tukachukue Kombe la Azam Federation Cup.

“Kikubwa tunataka mwakani Polisi Tanzania ikaiwakilishe Tanzania katika mashindano ya kimatifa kwa maana ya Ligi ya Mabingwa au Kombe la Shirikisho Barani Afrika, hivyo lazima tuzishinde changamoto za kwenye mashindano yatakayotupa tiketi ya kufika huko,”anasema Matola.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles