NDOSHI NG’HWANI NA SHEILA KATIKULA, MWANZA
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongela ametoa saa tano kwa Jeshi la Polisi, na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwakamata waliohusika na wizi wa mitihani ya darasa saba uliofanyika Septemba 5 hadi 6 mwaka huu.
Agizo hilo alilitoa jana wakati akizumgumza katika kikao cha kazi kilichojumuisha maofisa wa elimu, wamiliki wa shule, walimu wakuu wa shule za msingi za serikali na binafsi na watedaji wa kamati mbalimbali za idara ya elimu.
Mongela alitoa saa tano kwa polisi na Takukuru kuwakamata waliohusika na wizi wa mitihani hiyo na kuwafikisha katika vyombo vya dola kwa ajili ya uchunguzi wa kina.
“Hadi kufikia saa sita mchana naomba polisi na Takukuru hakikisheni wote waliohusika na wizi wa mitihani wanakamatwa, mamlaka zao zitawakuta gereza la Butimba na kabla ya saa sita leo hii mchana nataka taarifa za kuwakamata ziwe zimefika ofisini kwangu.
“Lazima tuchukue hatua hatua kali kwa wahusika wa wizi huu ili kila mtu ajionee kwa macho madhara ya kujihusisha na ujinga huu, tunahitaji kila mmoja aone kitendo cha wizi wa mitihani ni kibaya pia iwe fundisho kwa wengine kwani shule hii ya Alliance mwaka jana ilikamatwa na imerudia tena kosa lile lile tena hatuwezi kulifumbia macho,” alisema Mongela.
Pia aliwataka wamiliki na wakuu wa Shule za jijini humo kufuata kanuni na taratibu za usimamizi zilizowekwa na Baraza la Taifa Mitihani(Necta) na watakaoshindwa kuzifuata vituo vyaovitafungwa kwani kufanya hivyo ni kuihujumu nchi na taifa kwa ujumla.
“Kituo chochote kitakachobainika kina dosari au dalili yoyote ya udanganyifu wa kuiba mitihani kitafungwa na kubaki kama kituo cha mazoezi ya ziada na mmiliki pamoja walimu watakaobainika kuhusika watafikishwa katika vyombo vya sheria,” alisema.
Aliongeza kuwa ulimwengu upo katika teknolojia ya hali ya juu kwa sasa na wakati huu tuliopo elimu ndiyo kila kitu hivyo taifa halitafikia malengo yake endapo halitatengeneza misingi bora ya elimu kwa sasa.
Mongela alitoa onyo kwa Afisa Elimu wa Mkoa huo, Michael Ligola na kumtaka ahakikishe vitendo hivyo havijirudii na endapo vitajirudia basi watamalizana ofisini.