27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

POLISI KUFUMULIWA, MSANGI, MISIME WATAJWA KUMRITHI SIRRO DAR 

Na Mwandishi Wetu-DAR ES SALAAM


SIKU moja baada ya Amiri Jeshi Mkuu Rais, Dk. John Magufuli, kumwapisha mkuu mpya wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro sasa jeshi hilo liko mbioni kufumuliwa.


Kufumuliwa huko kunahusisha makamanda wa polisi wa mikoa,wakuu upelelezi wa mikoa, wakuu wa  polisi wa wilaya na maofisa upelelezi.


Hatua hiyo inatokana na ahadi ya IGP Sirro aliyoitoa juzi Ikulu Dar es Salaam baada ya kuapishwa, kuwa anatarajia kurejesha nidhamu ndani ya jeshi hilo na kukomesha mauaji yanayoendelea mkoani Pwani.


Taarifa za ndani ya jeshi hilo, ziliiambia MTANZANIA jana,  kuwa baada ya kuapiashwa kwa IGP Sirro, alikwenda makao makuu ya polisi Dar es Salaam na kufanya kikao kizito na watendaji wa juu wa jeshi hilo kama moja ya mkakati wake wa kulisuka upya jeshi hilo.


Licha ya hali hiyo, inaelezwa katika siku za hivi karibu baadhi ya viongozi wa juu ndani ya polisi, wamekuwa wakitajwa na hata kuhusishwa na matumizi mabaya ya fedha, ikiwamo kuhamisha fedha za miradi kinyume cha taratibu.


“IGP Sirro, uteuzi wake umeleta mshtuko mkubwa ndani ya jeshi la polisi kwa muda mrefu alikuwa akitajwa kushika nafasi hii. Kwa hatua na vikao vinavyoendelea sasa ni wazi kabisa kuna mabadiliko makubwa yanakuja.


“Makamanda wengi wa polisi wanatajwa kutemwa, tutegemee kupata sura mpya maana wapo baadhi yao wamekaa kwenye mikoa muda mrefu na kujenga mitandao yao jambo ambalo halitakiwi kwa polisi,” alisema mtoa habari wetu.


Pamoja na hali hiyo, IGP Sirro hivi sasa yupo katika chekecheke ya mrithi wake wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, huku majina ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi Ahmed Msangi  na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, David Misime yakitajwa kwamba huenda yakachomoza kurithi nafasi hiyo.


Misime, aliwahi kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke na baadaye akahamishiwa Mkoa wa Dodoma, ambapo alifanikiwa kuzima matukio mbalimbali ya uhalifu, huku akisifika kwa uchapakazi kabla ya mwaka jana kurudishwa makao makuu.


Naye Kamanda Msangi ambaye amewahi kuwa Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam (ZCO), anatambulika kwa kazi zake kutokana na kuwa na msimamo madhubuti katika kile anachokiamini.


Tangu amehamishiwa Mkoa wa Mbeya kwenda Mwanza, amefanikiwa kutuliza hali ya hewa ya mkoa huo ambayo kulikuwa na matukio mengi yakiwamo ya uvamizi wa misikiti.


Juzi baada ya kuapishwa, IGP Sirro, alitaja vipaumbele vyake kuwa ni kupambana na uhalifu na kuboresha nidhamu ya utendaji ndani ya jeshi hilo.


Akizungumza baada ya kuapishwa Sirro alisema atahakikisha Watanzania wanaishi kwa amani na utulivu na kuboresha nidhamu kwa sababu bila nidhamu ni vigumu kupambana na uhalifu.


“Napata kigugumizi sababu ya furaha, namshukuru Rais kwa kuniamini na kunipa nafasi hii, amewiwa na utendaji wangu.
“Kazi yetu kubwa ni kulinda watu na mali zao, nawaomba wananchi wanipe ushirikiano, uhalifu hauwezi kupungua kwa kutegemea Jeshi la Polisi peke yake,” alisema Sirro.


Kuhusu mauaji yanayoendelea mkoani Pwani, alisema kunahitajika nguvu ya pamoja kuweza kuishinda vita hiyo.
“Najua tuna changamoto kubwa ya Ikwiriri, Rufiji na maeneo mengine ya Pwani, tuko vizuri na tutaingia kufanya kazi kuhakikisha kwamba Wanapwani wanaishi kwa amani na utulivu.


“Wananchi watuamini, watupe taarifa kwa sababu ‘information is power’, wasipotupa taarifa itakuwa ni kazi ngumu,” alisema.

DALILI ZA MABADILIKO


Taarifa za ndani zinaeleza mabadiliko hayo yanakuja, huku jeshi la polisi likikabiliwa na changamoto nyingi, ikiwamo wizi wa silaha na mauaji ya raia na polisi katika matukio mbalimbali.

Serikali, vyama vya siasa na raia katika wilaya za Mkuranga, Rufiji na Kibiti mkoani Pwani.
Matukio ya majambazi kuvamia vituo vya polisi na kuua yalionekana wazi kumkera Rais Dk. Magufuli ambaye alilitaka jeshi hilo kudhibiti ili kukomesha vitendo viovu katika taifa.


Juni 25, mwaka jana, wakati wa uzinduzi wa Mpango wa Usalama wa Jamii, Rais Dk. Magufuli alisema: “Inashangaza jambazi anavamia kituo cha polisi anaua na anaondoka wakati polisi wapo na wana silaha na risasi wanazo, lakini wanashindwa kumnyang’anya silaha,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles