30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Pluijm atamba Tuzo VPL zampa jeuri

YANGA

NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa Yanga, Hans van der Pluijm, amesema uwepo wa wachezaji wengi wa timu hiyo katika kinyang’anyiro cha kuwania tuzo za Ligi Kuu Bara msimu uliopita, utaongeza ari ya ushindi kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Wachezaji watano wa kikosi cha Yanga wameingia kuwania tuzo katika vipengele tofauti ambapo beki Juma Abdul anapewa nafasi kubwa kwenye kinyang’anyiro cha kuwania mchezaji bora huku kipa Benno Kakolanya aliyeichezea Tanzania Prisons akichuana kwa upande wa kipa bora.

Nyota wa kimataifa wa Yanga, Donald Ngoma na Thabani Kamusoko, wanachuana vikali katika kipengele cha kuwania tuzo ya mchezaji bora wa kigeni huku mshambuliaji Mrundi, Amissi Tambwe, akisubiri zawadi yake ya kuibuka mfungaji bora kwa kufunga mabao 21.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Pluijm alisema mbali na kuwaongezea hamasa ya ushindi katika michezo ya kimataifa, pia kitendo cha majina yao kupendekezwa kuwania tuzo mbalimbali ni jambo la heshima kwa mabingwa hao wa Ligi Kuu msimu uliopita.

Alisema hamasa hiyo itawaongezea wachezaji hali ya kujiamini zaidi na kudhihirisha uwezo wao katika mechi za Kundi A za Kombe la Shirikisho Afrika zinazowakabili baada ya kupoteza dhidi ya Mo Bejaia ya Algeria na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Mholanzi huyo alisema Yanga inatarajia kushuka katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam Julai 16, mwaka huu kuivaa Medeama ya Ghana, mchezo ambao amedai unahitaji nguvu, akili na mbinu ili kuibuka na ushindi.

“Nimefurahi sana kwa kuwa thamani ya kikosi cha Yanga imeongezeka pia kwa mchezaji mmoja mmoja, ni jambo la furaha kwangu kuona wachezaji wa timu ninayofundisha wanapendekezwa kuwania tuzo muhimu,” alisema Pluijm.

Hafla ya kukabidhi tuzo, medali na fedha kwa washindi mbalimbali waliong’ara msimu uliopita wa 2015/2016 inatarajiwa kufanyika Julai 17, mwaka huu huku kocha Pluijm akipewa nafasi kubwa katika kipengele cha kuibuka kocha bora.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles