23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

PINDA AIBUKIA KANISANI RUKWA

 Na WALTER MGULUCHUMA-  KATAVI


WAZIRI Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda, amesema kuwa hajazeeka na bado anazo nguvu za kuchangia katika maendeleo ya  taifa licha ya kuwa amestaafu kazi  serikalini.

Akizungumza katika Ibada ya misa takatifu katika Kanisa la Maria Imamakulata, Jimbo Katoliki la Mpanda, Pinda alisema bado ana uwezo wa kuchangia katika taifa na jamii kwa kuwa ana afya njema.

Mbali na hilo, Pinda aliwaeleza waumini hao kuwa amefanya kazi serikalini kwa miaka 40, hivyo ni jambo la kumshukuru  Mungu kwa kipindi hicho chote  alichofanya kazi. 

“Katika kipindi cha utumishi  nikiwa serikalini, miaka ishirini na mbili   nimefanya kazi nikiwa Ikulu na miaka  15 kazi ya siasa, yaani ubunge pamoja na  miaka mitatu nimefanya katika Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali,” alisema Pinda.

Aidha aliwaomba viongozi wa dini  wawaombee viongozi wa Serikali wawe  na nguvu na afya za kuliongoza taifa na pia   waiombee nchi amani na utulivu izidi  kuendelea.

Pinda aliwataka waumini wa kanisa  hilo  kuwapeleka watoto wao kusoma katika Seminari ya Mtakatifu Paulo ili jimbo hilo  liwe na mapadri wengi, huku akieleza kuwa amevutiwa na matokeo ya ufaulu kwa kidato cha pili kwa miaka miwili  mfululizo.

Naye Paroko wa Kanisa hilo, Monsinyori   George Kisapa, alimshukuru Pinda kwa  michango yake mbalimbali ya maendeleo  aliyoitoa kwenye jamii na kwenye kanisa wakati na baada ya uongozi wake.

Alisema anaungana na Pinda kuwataka wazazi wawapeleke watoto wao kusoma shule za seminari  ingawa si  lazima kila anayesoma huko atakuwa padre.

Alisema seminari inasaidia kwa kiasi kikubwa kupata viongozi bora wa baadaye kama alivyokuwa waziri huyo mstaafu, ambaye alisoma katika Seminari ya Kaengesa mkoani Rukwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles