22.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

PENGO KATI YA MATAJIRI, MASIKINI LASHIKA KASI DUNIANI

Mtzd Design Friday templateSiah.indd

NA JOSEPH HIZA,

JUZI Jumanne umeanza mkutano wa siku tano, ambao umekuwa ukifanyika kila mwaka tangu 1971 katika eneo la mapumziko la Davos nchini Uswisi.

Mkutano huo maarufu kama jukwaa au kongamano la kimataifa la kiuchumi hukutanisha viongozi wa kisiasa na kibiashara kutoka kona zote za dunia.

Ni mkutano wenye kukutanisha watu wengi  wenye mawazo na mitizamo tofauti, wanasiasa, wafanyabaishara  na  wawekezaji.

Lakini pia hujumuisha wataalamu, asasi za kijamii na wanaharakati wa masuala ya  kijamii.

Kwa maneno mengine ni jukwaa lenye kuwaleta pamoja wanasiasa wenye madaraka makubwa zaidi na ushawishi, waandamizi wa masuala ya kifedha na viongozi wakubwa wa kibiashara.

Na  hapa  pia  kila mwaka  kunahubiriwa kuhusu  utandawazi zaidi, kufungua  mipaka ya biashara na  kuondoa vizuizi vya uwekezaji wa soko la hisa ili kuiweka dunia katika  mahali bora zaidi.

Hivyo, wanasiasa wa ngazi ya juu, viongozi mbali mbali wa kiuchumi na wanasayansi wa masuala ya kiuchumi zaidi ya 3,000 wanakutana.

Katibu Mkuu  mpya  wa  Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres anahudhuria jukwaa  hilo.

Mashirika yote muhimu ya kimataifa pia yanawakilishwa katika mkutano huo huku Kansela wa Ujerumani, Angel Markel akikosekana kutokana na kile kilichoelezwa kubanwa na matukio mengine ya kikazi.

Badala  yake, waziri wake wa  Fedha, Wolfgang Schaeuble na Waziri wa Ulinzi, Ursula von der Leyen watawakilisha.

Rais wa Ufaransa, Francois Hollande amebakia nyumbani na kadhalika Waziri Mkuu mpya wa  Italia, Paolo Gentiloni huku Waziri Mkuu wa Uingereza Theresa May akitarajia kuwapo.

Wanasiasa muhimu kutoka  Marekani hawatakuwapo mwaka huu, kwa kuwa Rais mteule Donald Trump anaapishwa Januari 20 mwaka huu, ambayo  ndio siku ya mwisho ya kongamano hili.

Ni meneja wa zamani tu wa  mifuko ya uwekezaji mbadala,  Anthony Scaramucci  anayetarajiwa kuwapo. Huyu ni mtu aliyetayarisha sehemu ya timu ya Trump ya kipindi cha  mpito inayomwandalia mazingira ya kuingia Ikulu ya Marekani, White House.

Moja ya ajenda muhimu zinazoelekea kutawala ni kujitoa kwa Uingereza EU (Brexit), China na utawala mpya wa Marekani chini ya Trump.

Hata hivyo, kuelekea mkutano huo kuna kikubwa kilichoshtua wengi na kuhitaji kuangaziwa zaidi na mkutano huo.

Ni ripoti ya kuendelea kuongezeka kwa pengo kati ya matajiri na maskini kwa kiwango, ambacho hakikufikiriwa kabla.

Hivyo basi, macho na masikio yataelekezwa Davod kuangalia namna litakavyopewa kipaumbele na kutafuta usumbuzi.

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Kukabiliana na Umasikini la Oxfam la Uingereza, pengo lililopo ni kubwa kuliko ilivyodhaniwa awali huku watu wanane kuanzia Bill Gates hadi Michael Bloomberg wakimiliki utajiri sawa na wa watu bilioni 3.6.

Ripoti inasema pengo kati ya watu matajiri zaidi na maskini ni kubwa zaidi kuliko ilivyokuwa mwaka mmoja uliopita na hivyo kuwahimiza viongozi kufanya mengi zaidi kuliko kuishia na maneno matupu.

Ripoti hiyo imeonya kuwa iwapo hali hiyo haitasawazishwa, ghadhabu ya umma kutokana na hali hiyo zitaendelea kupanda na kusababisha mabadiliko ya kushtua ya kisiasa.

Lilitolea kwa uchache mabadiliko ya kushtusha ikiwa ni pamoja na kuchaguliwa mtu wa Kalba ya Donald Trump kuwa rais wa Marekanina kura ya kujiondoa kwa Uingereza katika Umoja wa Ulaya.

Hilo linazua swali kubwa katika mataifa ya magharibi iwapo utandawazi unaohubiriwa sana katika mkutano huo na dunia ya kibiashara kwa ujumla pamoja  na ushindani wa kimataifa kama umeleta mafanikio yoyote.

Ni kwa sababu utandawazi umedaiwa kusababisha kukua kwa pengo hilo na matokeo yake ni ghadhabu za wapiga kura dhidi ya serikali zao na hivyo kusababisha uamuzi kama Brexit na ujio wa Trump, ambaye amezua hofu ya vita ya kibiashara au kujitenga.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Oxfam, Winnie Byanyima ambaye anahudhuria mkutano huu, ni hali ya kutatiza kwa utajiri mkubwa kuwa mikononi mwa watu wachache.

Mbaya zaidi mtu mmoja kati ya watu 10 anaishi kwa dola mbili kwa siku.

Anaongeza kuwa hali ya kutokuwa na usawa inawakwamisha watu wengi katika umaskini, kuharibu jamii na kudhoofisha demokrasia.

Ripoti kama hiyo ya mwaka mmoja uliopita ilisema kuwa watu 62 duniani wanamiliki utajiri sawa na watu wa tabaka la chini ambao ni nusu ya wakazi wote duniani.

Hata hivyo, Oxfam limekadiria upya idadi hiyo kufikia watu wanane kutokana na taarifa mpya zilizokusanywa na kitengo cha mikopo cha Benki ya Uswisi.

Shirika hilo la Oxfam pia lilitumia orodha ya mabilionea waliotathiminiwa na Jarida la Forbes katika taarifa yake ya Machi 2016 kutoa ripoti yake hiyo.

Kwa mujibu wa orodha hiyo ya Forbes, Bill Gates ndiye mtu mwenye utajiri mkubwa zaidi akikadiriwa kuwa na utajiri unaofikia dola bilioni 75.

Wengine katika orodha hiyo ni Amancio Ortega, mwanzilishi wa jumba la mitindo la Inditex nchini Hispania.

Wengine ni mfanyabiashara wa Marekani Warren Buffet, mfanyabiashara kutoka Mexico, Carlos Slim Helu, Mkuu wa Shirika la Amazon Jeff Bezos.

Wengine ni mwanzilishi wa mtandao wa kijamii wa Facebook, Mark Zuckerberg, mmiliki wa kampuni ya Oracle Larry Ellison na aliyekuwa meya wa Jiji la New York Michael Bloomberg.

Oxfam liliorodhesha mikakati ambayo lilisema lina matumaini ikitekelezwa itasaidia kupunguza hali hiyo ya kutokuwa na usawa.

Baadhi ya mikakati hiyo ni kuhakikisha ushuru wa juu kwa mali na mapato kuhakikisha kuwapo kwa usawa, pia kufadhili uwekezaji katika huduma za umma na ajira.

Aidha, ushirikiano bora miongoni mwa serikali katika kuhakikisha wafanyakazi wanalipwa vizuri na kwamba matajiri wanatakiwa kutokiuka ulipaji wa ushuru pamoja na viongozi wa kibiashara kujitolea kulipa kodi na kuwalipa wafanyakazi wao katika viwango bora.

Max Lawson, mshauri wa sera Oxfam, aliwahimiza mabilionea kufanya lililo sawa na kufanya kile ambacho Bill Gates amewataka wafanye ambacho ni kulipa ushuru.

Kwa mujibu wa rais na mkurugenzi mkuu wa shirika hilo, biashara huenda zikawa na msaada mkubwa wa kuimarisha uaminifu.

Kampuni zinahitaji kuwa na uwazi kwa wafanyakazi wake kuhusiana na mabadiliko yanayofanyika mahala pa kazi, kuimarisha utendaji kazi na kulipa viwango bora vya mishahara, sehemu ya mapendekezo ya ripoti hiyo inasema.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles