23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Nyama ya nguruwe yachangia ugonjwa wa kifafa – Daktari

Aveline Kitomary – Dar es Salaam

DAKTARI Bingwa wa Ubongo, Uti wa Mgongo na Mishipa ya Fahamu kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Patience Njenje, amesema ulaji wa nyama ya nguruwe ambazo hazijaivishwa vizuri, umekuwa ukisababisha ongezeko la ugonjwa wa kifafa kwa asilimia 15.

Dk. Njenje amesema hatari ya ulaji wa nyama hizo inatokana na wanyama hao kuwa na minyoo aina ya tegu ambayo ina uwezo wa kusasabisha uvimbe kwenye ubongo.

Akizungumza wakati alipokuwa akitoa elimu kwa jamii jana Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kifafa Duniani, Dk. Njenje alisema sababu zingine za ugonjwa wa kifafa kuongezeka ni ajali.

“Sababu za kifafa ziko nyingi, ajali inachangia kwa asilimia 10 mpaka 15 ya wagonjwa nchini, ongezeko linakuja kutokana na kuongezeka kwa aina ya usafiri wa bodaboda ambapo ajali inapotokea mtu huweza kuumia kichwa na  ukiumia kinachofuata ni ubongo kuwa na kovu, hivyo huko mbeleni unaweza kupata kifafa.

“Vivimbe ndani ya ubongo hivi viko vya aina nyingi, ila kuna viwili vikubwa. Kuna vivimbe vya minyoo na saratani, mfano ulaji wa nyama za nguruwe ambazo hazijaiva mtu anaweza akapata tatizo kwani ile kitimoto ina wadudu wa minyoo ambao wataingia ndani ya mwili na wataenda kwenye ubongo.

“Pia kuna minyoo kwa paka, kama kinga ikishuka wana uwezo wa kukushambulia na kupanda hadi kwenye ubongo, hivyo kupelekea  uvimbe, kingine ni uzazi wa shida, hii inasababisha kifafa kwa  asilimia 30, mfano mama akiwa na njia ndogo ya uzazi halafu mtoto akashindwa kutoka na hii huzuia hewa kwenye ubongo wa mtoto,” alisema Dk. Njenje.

Alisema utafiti uliofanyika hapa nchini unaonyesha katika kila watu 1,000 watu 37 wana tatizo la kifafa, huku zaidi ya watu milioni 60 wakikumbwa na tatizo hilo duniani.

“Kwa kila mwaka kuna ongezeko la watu 70 kati ya 100,000 duniani kote, hivyo kidunia ugonjwa huu una kasi kubwa, hasa kwa upande wa Afrika ugonjwa huu uko mbele mno ambapo katika kila watu 1,000 watu 50 wameathirika na kifafa, asilimia kubwa wanatoka Afrika.

“Tafiti zilizofanyika kama ule wa Mahenge, Morogoro wa ugonjwa wa  kifafa  kwa Afrika, Tanzania inaongoza, kwahiyo hili ni tatizo kubwa, wagonjwa wana hatari ya kufa mara sita zaidi ya mtu ambaye hana kifafa,” alibainisha Dk. Njenje.

Alisema kuwa asilimia 36 ya jamii wana imani potofu kuhusu ugonjwa huo, hali ambayo imesababisha wagonjwa wengi kutokufika hospitali kwa wakati au kutofika kabisa.

“Asilimia 50 ya jamii bado wanaamini kifafa ni ugonjwa wa kuambukizwa kitu ambacho si kweli, huku zaidi ya asilimia 75 ya wagonjwa wa kifafa wakienda kutafuta tiba kwa waganga waa kienyeji  na viongozi wa dini wakiamini kuwa ugonjwa huo unasababishwa na mashetani.

“Kwahiyo tunapoteza watu ingawa katika jamii watu wamekuwa wakiishi kwa mazoea na kuwa na imani mbalimbali kuhusu kifafa, wengine wanaamini sio ugonjwa wa kawaida, wanasema ni  kulogwa au majini,” alisema Dk. Njenje.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles