27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NMB yaahidi kuendelea kusaidia mendeleo ya elimu nchini

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Maafisa wa Benki ya NMB Kanda ya Kaskazini wamesisitiza dhamira ya benki hiyo kuendelea kusaidia kuweka mazingira rafiki ya kujifunzia shuleni kama sehemu ya kuunga mkono juhudi za kitaifa za elimu bora.

Meneja wa NMB tawi la Madaraka jijini Tanga – Elizabeth Chawinga akimkaribisha Afisa Mahusiano wa Wateja wa benki hiyo tawi la Madaraka Godfray Methew kuzungumzia huduma za bima zinazotolewa na benki hiyo kwenye Kongamano la Elimu lililofanyika jijini Tanga. Kongamano hili lilifanyika jijini Tanga mwishoni mwa juma.

Wakizungumza katika kongamano la elimu mjini Tanga wiki iliyopita, viongozi hao waliahidi kuwa NMB itaendelea kushirikiana na mamlaka za mkoa na taifa kuhakikisha viwango vya elimu nchini vinaimarika zaidi.

Meneja Mauzo wa NMB Kanda ya Kaskazini, Innocent Mwanga, alisema katika mahojiano wakati wa Kongamano la Wadau wa Elimu wa Mkoa wa Tanga kuwa kusaidia elimu ni wajibu wa benki hiyo kwa sababu sekta hiyo ni muhimili nyeti katika maendeleo ya taifa.

“Elimu bora ni swala la msingi katika kujenga jamii na nguvu kazi iliyopevuka kwa ajili ya maendeleo ya sekta mbalimbali za uchumi wa taifa. Ni kwa sababu hiyo Benki ya NMB ilikubali kufadhili kongamano hili ili tuwe sehemu ya juhudi za kusaidia kuboresha viwango vya elimu katika mkoa huu,” amesema Mwanga.

Kongamano hilo liliandaliwa na Kundi la WhatsApp la Sauti ya Tanga ili kuzichambua changamoto za elimu zinazokabili mkoa huo na kuangalia jinsi ya kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa Tanga katika mitihani ya kitaifa.

Nae Meneja wa NMB tawi la Madaraka la Jijini Tanga, Elizabeth Chawinga, alisema benki hiyo itaendelea kudhamini kongamano hilo litakalofanyika kila mwaka kama ishara na mfano wa kuendelea kusaidia maendeleo ya sekta ya elimu nchini.

Kwa mujibu wa Bw Mwanga, ushiriki wa NMB katika maendeleo ya elimu umejikita zaidi katika uwekezaji wa kujenga na kuboresha miundombinu haswa kupitia ujenzi wa madarasa na michango ya samani mbalimbali.

Pia benki hiyo huwafadhili wanafunzi wa shule za sekondari na kutoa suluhisho za bima za elimu kwa ajili ya kulipa ada pale inapotokea walezi kufariki au kupata ulemavu wa kudumu.

Kufadhili elimu ni sehemu muhimu ya shughuli za uwajibikaji wa NMB kwa jamii (CSR) na kila mwaka utenga asilimia moja ya faida yake baada ya kodi kwa ajili ya uwekezaji huo.

Wakati wa uzinduzi wa asasi ya NMB Foundation na Programme ya Scholarship na Mentorship ya Nuru Yangu mwezi Septemba mwaka jana benki hiyo ilisema hutumia zaidi ya TZS bilioni moja kila mwaka kufadhili maswala ya elimu.

Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita uwekezaji mkubwa iliyofanya kwenye elimu ulinufaisha takriban shule 1,400 kote Tanzania kupitia vitu mbalimbali yakiwemo madawati 83,000 na kompyuta 1,200.

“Lengo letu kwa ujumla na nguzo ya msingi katika kuwekeza kwenye elimu ni kuwasaidia watoto wetu kutimiza ndoto zao kwa kuwatengenezea mazingira mazuri ya kujifunzia na kukua kitaaluma,” NMB inatabainisha kwenye ripoti ya uendeshaji wake ya mwaka 2020.

Ngeni rasmi kwenye kongamano hilo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Adam Malima, aliipongeza benki hiyo kwa kujitolea kwa dhati kusaidia maendeloe ya elimu na kuwataka wadau wengine kuiga mfano wake.

Kiongozi huyo alisema swala la msingi katika maendeleo ya elimu si ufaulu tu ila viwango vya ufaulu huo na ubora wa elimu inayotolewa.

Mawazo yake yalisisitizwa na mwenyekiti wa SAUTI, Mwantumu Mahiza, aliyesema wazo la kuandaa kongamano hilo lilichagizwa zaidi na kutaka kusaidia kuboresha elimu mkoani Tanga.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles