27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Ni mtikisiko

Mtanzania 190914NA WAANDISHI WETU

MTIKISIKO mkubwa wa kisiasa jana umelikumba taifa, baada ya wafuasi wa Chadema kupambana na polisi katika maeneo mbalimbali.

Hali hiyo, ilianza kuonekana mapema jijini Dar es Salaam, wakati Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliwapowasili Makao Makuu ya Jeshi la Polisi saa tano asubuhi kwa ajili ya kuhojiwa.

Mbowe aliitwa kuhojiwa na viongozi wa jeshi hilo kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi wiki iliyopita.

Akizungumza kwenye mkutano wa Kamati Kuu ya chama chake, Mbowe alisema wataitisha maandamano na migomo isiyokuwa na kikomo nchi nzima kuishinikiza Serikali kusitisha Bunge Maalumu la Katiba linaloendelea mjini Dodoma.

Mbowe aliwasili polisi saa 5 asubuhi akisindikizwa na msafara wa magari matano yaliyobeba baadhi ya wanachama, mawakili na viongozi wa chama hicho.

Baada ya kuwasili katika eneo hilo, wanachama hao walipinga kiongozi wao kushuka ndani ya gari hadi atakapoingia ndani ya lango kuu.

Wanachama hao walisikika wakisema ‘Peoples’ huku wengine wakiitikia ‘Power’.

Kitendo hicho kilipingwa na polisi waliokuwa wakilinda lango hilo na kuamuru Mbowe ashuke na kuingia kwa miguu ndani ya jengo hilo.

Kitendo hicho kilionekana kuwakera wafuasi waliokuwa wamekusanyika eneo hilo na kuamua kusukuma lango hilo kwa nguvu ili waweze kuingia pamoja na kiongozi wao.

Kutokana na hali hiyo, wafuasi hao waligoma na kuanza kupambana na polisi ambao nao walijihami kwa kuzuia geti la lango wakiwa ndani.

Baada ya mabishano ya muda mrefu, ndipo polisi walipokubali Mbowe aingie na gari ndani ya jengo hilo huku wakizuia msafara wa magari mengine.

Kutokana na uamuzi huo, mawakili walilazimika kushuka ndani ya gari.

Mmoja wa askari aliyekuwa getini hapo, alisikika akisema anayepaswa kuingia ndani ya jengo ni Mbowe na mawakili wake.

“Tumekubaliana gari linaloingia ndani ni moja tu la mwenyekiti, msilazimishe matumizi ya nguvu,” alisikika akisema askari huyo.

Kitendo hicho kilipingwa na wanachama hao huku wakitaka wabunge, mawakili na viongozi wengine waingie ndani.

Kutokana na hali hiyo, polisi walikubali na kuwaruhusu viongozi hao kuingia ndani huku wakiwaamuru wanachama wengine na waandishi wa habari kusimama umbali wa mita 200 kutoka kwenye lango hilo.

Baada ya kutokea kwa tangazo hilo, wafuasi hao walikaidi amri hiyo na kusababisha askari D. D. Zahoro kuamuru kutumika nguvu kuwatawanya pamoja na waandishi wa habari hali iliyosababisha kujitokeza kwa vurugu katika eneo hilo.

Vurugu hizo zilidumu kwa muda wa saa moja na kusimamisha shughuli mbalimbali zinazoendelea ndani ya jengo hilo na njia kufungwa kwa muda.

Katika vurugu hizo,wafuasi  wanne wa chama hicho walikamatwa.

MWANDISHI APIGWA

Katika tukio hilo, mwandishi wa habari wa Gazeti la Tanzania Daima, Josephat Isango alijikuta akishambuliwa vibaya na askari kwa virungu.

Licha ya Isango kuonyesha kitambulisho, polisi hawakutaka kumsikiliza zaidi ya kuendelea kumshushia kipigo na kumsababishia maumivu katika mguu wa kulia.

Kipigo hicho kilisitishwa baada ya waandishi wengine kupiga kelele kuwaomba polisi kumwachia kwa sababu  alikuwa kwenye majukumu yake ya kazi.

MBOWE AHOJIWA

Wakati tukio hilo likiendelea, Mbowe alikuwa ndani ya jengo hilo akiendelea kuhojiwa  akiwa na mawakili wake sita.

Mawakili hao, ni Peter Kibatala, Profesa Abdallah Safari, Mabere Marando, Nickson Tugala, Tundu Lissu na John Malya.

Mahojiano hayo yalianza saa tano na kudumu kwa zaidi ya saa nne. Ilipofika saa 8:49 mchana, mawakili wanne wakiongozwa na Lissu walitoka nje na kuzungumza na wafuasi na waandishi wa habari.

“Mwenyekiti yuko salama, aliitwa kwa ajili ya mahojiano na yamefanyika vizuri chini ya mawakili.

“Polisi wameomba tuzungumze na nyie tuwaombe muondoke kwa sababu mwenyekiti akitoka na mkiwa wengi kunaweza kukawa na uvunjifu wa amani,” alisema Lissu.

Baadhi ya wanachama hao walisikika wakisema hawawezi kuondoka kwa sababu hawawaamini polisi.

“Sisemi nawaamini polisi au la, tumekubaliana kwamba mwenyekiti atapata dhamana, hivyo haitakuwa busara tukiondoka kwa maandamano, tulikuja kwa amani hatutaki mtu atoke hapa akiwa amedhurika,” alisema Lissu.

Baadhi ya wafuasi walikubali kuondoka huku wengine wakibaki.

Saa 9:17 alasiri, Mbowe alitolewa kwa kupitia mlango wa nyuma wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, huku akisindikizwa na magari manne kwenda Kituo cha Polisi Kati ambako  aliachiwa kwa dhamana.

MTIKILA
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila alifika eneo hilo akiwa kwenye bajaj, lakini alizuiwa kuingia ndani.

DODOMA

Polisi mjini Dodoma, jana waliimarisha ulinzi kwa ajili ya kupambana na wafuasi wa Chadema waliopanga kuandamana kupinga Bunge Maalumu la Katiba linaloendelea mjini humo.

Miongoni mwa maeneo yaliyokuwa na ulinzi mkali ni pamoja na jengo la Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Viwanja vya Nyerere Square na mitaa mbalimbali ya mjini hapo.

Polisi waliweka uzio wa kamba kilipo Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) na makutano ya barabara jirani na stendi ya mabasi ya abiria yanayokwenda mikoani ili kutoruhusu watu na magari kuelekea eneo la Bunge.

Jengo la Bunge lilikuwa limezungukwa na askari wengi wenye silaha, farasi na mbwa kuhakikisha usalama unakuwapo katika eneo hilo.

Ndani ya eneo la Bunge, nako ulinzi ulikuwa mkali kwani kulikuwa na idadi kubwa ya askari waliokuwa na silaha pamoja na mbwa.

Viwanja vya Nyerere

Katika viwanja vya Nyerere ambako wakazi wa Dodoma hupenda kukusanyika kwa ajili ya kupumzika na kupata huduma za chakula na vinywaji, jana shughuli zilisimama kwa muda kwa kuwa polisi walikuwa wameweka ulinzi tangu asubuhi.

Nje ya viwanja hivyo, kulikuwa na vijana waliokuwa na mabango likiwamo lililosomeka ‘Sitta tumia busara ahirisha Bunge la Katiba’.

Katika viwanja hivyo, polisi walionekana wakiwa wamekamata vijana wapatao kumi waliodaiwa kuwa walikuwa wakitaka kuandamana.

Wakati hali ikiwa hivyo katika maeneo hayo, ulinzi pia uliimarishwa katika mitaa mbalimbali ya mji huo kwani askari polisi waliokuwa na silaha na askari kanzu, walikuwa wametanda kila kona.

Chini ya ulinzi huo, magari yaliyokuwa yamejaa askari polisi yakiwamo ya askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), yalikuwa yakizunguka kila kona kuhakikisha hakuna maandamano yatakayofanyika.

Gari la Chadema

Pamoja na askari kuimarisha ulinzi huo, gari la Chadema lenye namba za usajili T 792 CAX likiwa na nembo ya M4C, nalo lilikuwa likipita katika mitaa ya mji huo ingawa haikufahamika lilikuwa likifanya hivyo kwa maana gani.

Kuanzia saa 12 alfajiri jana, ofisi za Chadema Mkoa wa Dodoma zilizoko eneo la Mji Mpya, zilikuwa zikilindwa na askari polisi waliokuwa na silaha.

Radio za kijamii zafungwa

Katika hali ambayo haikujulikana wazi, radio za kijamii za mjini hapa hazikuwa hewani jana asubuhi kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kudhibiti mawasiliano kati ya Chadema na wananchi.

Taarifa zilizopatikana baada ya mawasiliano hayo kukatika, zinasema redio hizo hazikuwa hewani kwa saa kadhaa jana kwa vile viongozi wa Chadema walikuwa wakizitumia kuhamasisha wananchi.

Miongoni mwa waliodaiwa kutumia redio hizo ni Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Dodoma, Jella Mambo ambaye awali alihamasisha maandamano hayo kupitia Redio Kifimbo na Nyemo FM.

Hata hivyo, taarifa nyingine zinasema redio hizo hazikuwa hewani kwa kuwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) walikuwa wakifanya marekebisho ya masafa.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mambo alikiri kutumia redio hizo kuhamasisha maandamano kwa kuwa yalikuwa halali.

Pamoja na hayo, alisema kama Jeshi la Polisi limedhamiria kudhibiti maandamano yao, linatakiwa kuandaa fedha nyingi ili kukabiliana nayo.

“Hapa Dodoma maandamano yapo ila tunayafanya kimkakati kwani watu wametawanyika maeneo mbalimbali kila mmoja ana mabango yenye ujumbe tofauti, yakiwamo tunayompongeza Rais Jakaya Kikwete kwa busara yake aliyoitumia kutaka mchakato wa Katiba Mpya usikamilike kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015,” alisema Mambo.

Wakati huo huo, Mambo alisema gari moja la Chadema lililokuwa limebeba wajumbe wa Mkutano Mkuu waliokuwa wakitoka Dar es Salaam kuelekea Mwanza, lilikamatwa na askari polisi.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Emannuel Lukura alikiri kukamatwa kwa gari na wafuasi wanne wa chama hicho.

MBEYA

Habari kutoka mkoani Mbeya, zinasema polisi wameendelea kutunushiana misuli na Chadema kuhusu kufanyika au kutofanyika kwa maandamano ya kupinga kuendelea kwa Bunge Maalumu la Katiba.

Chadema imesisitiza kufanyika kwa maandamano hayo leo. Mratibu Kanda za Nyanda za Juu Kusini, Franky Mwaisumbe aliliambia MTANZANIA jana kuwa licha ya polisi kudai kuwa maandamano hayo ni batili, wao watahakikisha yanafanyika kwani lengo lao ni kufikisha ujumbe kwa wananchi.

Alisema wao wanachokifanya ni kutimiza azimio la Kamati Kuu lililotolewa wiki iliyopita na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, alisema hadi jana jioni maandamano hayo yalikuwa hayajaombewa kibali.

ARUSHA

Mkoani Arusha, Chadema kimethibitisha kufanya maandamano leo, huku kikisema tayari majimbo 14 kati ya 33 yamewasilisha barua katika vituo vya polisi kwa ajili ya taarifa.

Katibu wa Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa akizungumza na MTANZANIA kwa njia ya simu jana, alisema tayari wamekwishajipanga kuhakikisha wanafanya maandamano ya amani ambayo hayatasababisha usufumbufu kwa watu wala kuvunja sheria yoyote.

“Lengo letu ni ujumbe ufike kwa wabunge Dodoma, kwamba kikao wanachoendelea nacho hakitatupa Katiba mpya. Sasa maandamano haya tumeyapa kwa mfumo wa pekee kabisa,” alisema.

Habari hii imeandaliwa na Patricia Kimelemeta, Nora Damian na Shabani Matutu (Dar es Salaam),  Maregesi Paul, Rachel Mrisho na Debora Sanja (Dodoma), Pendo Fundisha (Mbeya) na Elia Mboneya (Arusha).

- Advertisement -

Related Articles

2 COMMENTS

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles