25.8 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Ni kweli hatuwajui wauza ‘unga’?

ungaNA SARAH MOSES

TUMEKUWA tukishuhudia watumiaji wa dawa za kulevya maarufu wakiongezeka na kusababisha nguvu kazi ya taifa ambayo ni vijana kupungua.

Mkoani Dodoma, watumiaji hao wamekuwa wakizagaa na kusababisha kero kwa watu wanaotumia barabara ya mitaa ya Airport, Kata ya Viwandani kwani wamekuwa wakilewa na kusinzia barabarani.

Wengine wamekuwa wakisaidiwa kwa kupewa elimu na hatimaye huacha kuyatumia, lakini kwa Dodoma hili halipo.

Wengi wa watumiaji wa dawa hizo ni vijana  wadogo ambao walitakiwa kuwapo shuleni na wengine katika shughuli za kujenga taifa.

Hivi karibuni katika maeneo hayo, vijana hao walikumbwa na ugonjwa wa kuharisha baada ya kudaiwa kuwa mhusika anayewauzia unga kuwaambia kuwa umeisha.

Hali hiyo ilisababisha kujazana katika eneo hilo huku wengine wakilia wakidai kuwa wana kiu.

Haya ni baadhi tu ya matukio ya watumiaji wa dawa za kulevya, swali ni je, wahusika hawa wanaouza dawa hamuwajui au ndiyo funika kombe mwanaharamu apite?

Na kama mnawafahamu ni hatua gani stahiki zinachukuliwa ili kuwanusuru vijana hawa ambao ni taifa la kesho.

Watumiaji hawa wa dawa za kulevya ni zao la watoto wa mitaani ambao wamekuwa wakizagaa mjini hapa hasa katika eneo la Nyerere Square, huku wakiwa na chupa za maji safi ambayo ndani yake yana dawa za kuwalewesha wanazonusa kila wakati.

Watoto hao ambao wengi wao wanaanzia umri wa miaka mitano hadi 15, umri ambao walitakiwa kuwepo shuleni.

Kumekuwa na vituo vingi vya kulelea watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu vikiwasaidia vijana hao lakini hawa wanaotumia unga wameachwa hadi wanafikia hatua ya kujihusisha na wizi na kuomba omba mitaani.

Watoto hao wamekuwa wakipita kwenye mabaa, benki na sehemu nyingine zenye mikusanyiko ya watu wakiomba fedha huku wakiwa na chupa zao puani.

Eneo la Nyerere Square ni maalumu kwa ajili ya watu kupumzika na kubadilishana mawazo, lakini limegeuka kero kutokana na usumbufu wa watoto hao wa mitaani kuwasumbua watu kwa kuomba omba.

Wakati mwingine, watoto hawa huwatukana watu baada ya kuomba fedha na kunyimwa bila kujali umri wa mtu huyo. Hii inamaanisha hawana maadili na yanazidi kupotea kutokana na kutokuwa na uangalizi.

Ikumbukwe kuwa wanavyoachwa waendelee nao wanazidi kuhamasisha watoto wenzao wengine kujiunga na makundi ya namna hiyo.

Pamoja na mambo mengine, watoto hawa pia wamekuwa na tabia ya kulawitiana  wenyewe kwa wenyewe na watu wazima wanaoambatana nao na kuambukizana magonjwa.

Tukumbuke vijana ndiyo nguzo ya taifa na watoto ni taifa la baadaye, hivyo basi tusipokuwa makini na kuweka sheria ambazo zitambana kila mtu, tusipowatengeneza vijana na watoto hawa mapema siku moja tutashikana mashati wenyewe kwa wenyewe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles