30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NENO ‘NUSU KAPUTI’ LAMKERA KIGOGO DAR


NA VERONICA ROMWALD - DAR ES SALAAM  |  

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Mpoki Ulisubisya ameishauri jamii kuacha kutumia neno ‘nusu kaputi’ na badala yake watumie tiba ya dawa za usingizi.

Akizungumza Dar es Salaam jana wakati akifungua mafunzo ya awamu ya tatu kwa wataalamu wa dawa za usingizi, alisema neno hilo huwaogopesha wagonjwa wanaotakiwa kufanyiwa upasuaji.

“Sijajua kihistoria neno kaputi linapotoka lakini haraka haraka maana yake ni kwamba mtu amekufa, hivyo unaposema nusu kaputi maana yake umeua mtu nusu na nusu nyingine bado yupo hai.

“Sasa hii inawaogopesha sana wagonjwa, tungependa jamii itambue kwamba fani hii inatoa dawa ya kulaza wagonjwa au dawa ya usingizi ili mtu asisikie maumivu wakati akipasuliwa kwani huwa anakatwa na anahisi maumivu,” alisema.

Alisema ndiyo maana wataalamu wanaotoa tiba hiyo wanatambulika kama wataalamu wa tiba ya usingizi na si wataalamu wa nusu kaputi.

“Ili kuondoa ule woga, kusudi mtu ajue anakwenda kule anapewa dawa ya usingizi na tunajua mtu anapolala kuna kuamka, ndiyo maana tunapenda neno hili, sisi tunatoa dawa ya usingizi na mtu anaamka baada ya upasuaji,” alisema.

Alisema fani ya utoaji dawa kwa ajili ya wagonjwa wanaohitaji kufanyiwa upasuaji ni sawa na fani zingine za afya ambazo mtu lazima ajifunze, afanye mazoezi ya kutosha ndipo akafanye kazi husika.

“Mara nyingi watu ambao hawajasoma kwa muda mrefu, wanaweza kufundishwa kazini na watu waliobobea au wanasoma mwaka mmoja, wengine mitatu au hadi saba.

“Sasa inategemea mwaka aliosoma kunaweza kuwapo mambo ambayo yalifaa kwa muda ule lakini leo hii yanazidi kubadilika, ndiyo maana tunahitaji mafunzo ya namna hii mara kwa mara ili kuwajengea uwezo wa mtaalamu wa kisasa,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles