25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

NEMC yasisitiza matumizi ya nishati jadidifu

Na MWANDISHI WETU-MOROGORO



BARAZA  la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), limehimiza matumizi ya nishati jadidifu ili kuhakikisha kwamba ujenzi wa viwanda nchini hausababishi athari kubwa kwa  mazingira.

Hatua hiyo inatokana na mpango wa Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati na viwanda ifikapo mwaka 2025 na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais Dk. John Magufuli imejidhatiti kutimiza azma hiyo.

Akizungumza mjini hapa mwishoni mwa wiki, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dk. Vedast Makota alisema Baraza lake linafanya kazi na wadau mbalimbali kuhakikisha kwamba utekelezaji wa miradi ya kuzalisha umeme kwa ajili ya uchumi wa viwanda unafanywa kwa namna ambayo haitaleta athari kwa mazingira.

Dk. Makoto alikuwa anazungumza katika semina ambayo imewakutanisha wataalamu wa mazingira na nishati zaidi ya 70 kutoka NEMC, Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na Halmashauri za Wilaya na Majiji kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Pwani na Tanga.

“Kwa kuelewa kwamba Tanzania inahitaji kuzalisha umeme mwingi ili kuongeza uwezo wake wa kuweza kuhimili ongezeko la viwanda, tumeamua kuja na kufanya mazungumzo na wataalamu hapa kwa lengo la kuhakikisha kwamba wanakuwa mstari wa mbele katika kutekeleza majukumu yao katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya uzalishaji wa umeme,” alisema Dk. Makota

Alisema duniani kote, nchi zinaibua miradi rafiki kwa mazingira kwenye uzalishaji wa nishati ili kuhakikisha kwamba ukuaji wa uchumi hauleti matokeo hasi katika juhudi za kutunza na kuhifadhi mazingira.

“Ukuaji wa uchumi hauwezi kuwa endelevu kama utagharimu usalama wa mazingira yetu…..hii ndiyo sababu tunahimiza uendelezaji wa nishati jadidifu kama nishati ya jua, uwepo, joto ardhi na maji…..,” alisema.

Kwa Mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha Usimamizi wa Mazingira cha Wizara ya Nishati, Innocent Makomba, Tanzania ina uwezo wa kuzalisha hadi Megawatts 4.7 za umeme kutoka kwenye vyanzo vya nishati jadidifu vilivyopo.

Kwa sasa, alisema, nchi inazalisha kiwango kinachokadiriwa kufikia 500 na 800 Megawatts kutoka kwenye gesi na maji mtawalia, na akaongeza kwamba uwezo uliopo ni mkubwa zaidi.

“Hii ndiyo sababu tunazungumzia ushirikishwaji wa sekta binafsi kwenye uzalishaji wa nishati kwa kutumia vyanzo vya nishati jadidifu,” alisema

NEMC imekuwa ikilipa msukumo mkubwa suala la uhifadhi mazingira huku ikihamasisha uwekezaji rafiki unaozingatia kuweka mazingira endelevu katika uwekezaji kwa faida na manufaa ya vizazi vijavyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles