26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NEC yatoa utaratibu uandikishaji wapiga kura

Na NORA DAMIAN

-DAR ES SALAAM

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imesema uboreshaji Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, unatarajia kuanza Julai kwa kutumia teknolojia ya kielektroniki.

Uboreshaji huo utawahusu wapiga kura wapya waliotimiza miaka 18 na wale watakaotimiza umri huo wakati wa uchaguzi mkuu wa mwakani.

Akizungumza jana wakati wa mkutano na wadau kutoka asasi za kiraia, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Semistocles Kaijage, alisema  kundi lingine litakalohusika ni wale watakaoboresha taarifa zao kama waliopoteza kadi au kadi zao kuharibika na waliohamia maeneo mengine ya uchaguzi.

“Baada ya uchaguzi wa mwaka 2015 tume iliendesha zoezi la uhakiki katika vituo vya kuandikisha wapiga kura nchi nzima, lengo ni kujua kama bado vina hadhi ya kuwa vituo vya kuandikisha wapiga kura kwa mujibu wa sheria,” alisema Jaji Kaijage.

Alisema kwa upande wa Tanzania Bara waliongeza vituo vya kuandikisha wapiga kura kutoka 36,549 hadi 37,407 na kwa Zanzibar vituo vimeongezeka kutoka 380 hadi 407.

Mwenyekiti huyo wa NEC alisema pia Machi waliendesha zoezi la uboreshaji wa majaribio katika Kata ya Kihondo mkoani Morogoro na Kata ya Kibuta mkoani Pwani ambapo walifanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Hata hivyo alisema kulikuwa na changamoto ndogondogo ikiwemo ya wapiga kura kutokuwa na uhakika wa kumbukumbu za majina yao.

“Tume itatoa vibali kwa baadhi ya asasi za kiraia kutoa elimu ya mpiga kura wakati wa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

“Hivyo tume imeaandaa mwongozo wa utoaji wa elimu hiyo, asasi za kiraia zitatakiwa kuufuata wakati wote wa uelimishaji umma kuhusu uboreshaji huo,” alisema.

Alisema katika uchaguzi wa mwaka 2010 asasi za kiraia 66 zilipewa vibali na katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 asasi 447 zilipewa vibali vya kutoa elimu. 

Jaji Kaijage alisema tume inatambua umuhimu wa kuwashirikisha wadau katika mchakato wa uchaguzi kwa lengo la kuwa karibu nao na kuweka uwazi katika utekelezaji wa majukumu yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles