27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NEC kutofuata sheria kunakosesha watu imani na uchaguzi

Na Margareth Chambiri -Dodoma


TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imewataka wasimamizi wa uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika Desemba 3 kufuata sheria na kutenda haki kwa vyama vyote.

Imesema  kutofanya hivyo huharibu imani ya wadau na kusababisha malalamiko ya kutoridhishwa na mchakato wa uchaguzi.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa NEC, Dk Athumani Kihamia,  alipofungua mafunzo kwa wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi   Dodoma.

Ametoa kauli hiyo wakati vyama mbalimbali vikiwa vimegomea uchaguzi huo vikisema  uchaguzi mdogo uliofanyika nchini hivi karibuni haukuwa  huru wala wa haki.

Jana, Dk. Kihamia alisema watendaji wote wa tume wanapaswa kuwapo katika maeneo yao ya kazi wakati wote hususan kipindi cha uteuzi.

Aliwataka kufungua ofisi   muda wote ambao umeruhusiwa kwa mujibu wa sheria ili vyama vyote vinavyoshieiki  vipewe fomu za uteuzi na wagombea wao wateuliwe kama wamekidhi vigezo.

Alisema  kutozingatiwa mambo hayo husababisha kuharibu imani ya wadau na malalamiko ya kutoridhishwa na mchakato wa uchaguzi na hatimaye mashauri ya uchaguzi kufikishwa mahakamani.

Dk. Kihamia amewataka wasimamizi na wasimamizi wasaidizi hao wa uchaguzi kutojihusisha na migogoro  ndani ya vyama.

Alisema  iwapo vyama vitakuwa na malalamiko vielekezwe kuwasilisha malalamiko yao kwenye Kamati za Maadili na si mahali pengine popote.

Kwa mujibu wa Dk. Kihamia, uchaguzi wote duniani ni kielelezo cha demokrasia na   uchaguzi huru na wa haki hutokana na wasimamizi wa uchaguzi wanaozingatia sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia uchaguzi husika.

Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Mbarouk Salum Mbarouk, aliwataka wasiamamizi hao kuacha kufanya kazi kwa mazoea kwa sababu  sheria ya Taifa ya Uchaguzi na ile ya Serikali za Mitaa zinaunda kosa la jinai na kutoa masharti ya adhabu kwa ofisa yeyote wa uchaguzi ambaye atasababisha kuharibu uchaguzi.

Aliwataka wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi kuyaelewa vema maeneo wanayofanyia kazi na kujiamini.

Vilevile  amewakumbusha jukumu walilo nalo la kuimarisha imani ya wananchi na wadau wengine wa uchaguzi kwa NEC.

Wasimamizi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi 210 kutoka majimbo manne ya Serengeti, Simanjiro, Ukerewe na Babati Mjini na kata 47 zinazotarajiwa kufanya uchaguzi mdogo Desemba 3, wanashiriki katika mafunzo hayo ya siku tatu   Dodoma.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles