25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Ndugai asema Mbowe ni mtoro bungeni

RAMADHAN HASSAN-DODOMA

SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amedai nafasi ya kuuliza swali la kwanza katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu bungeni imekuwa ikipotea kutokana na utoro wa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.

Alitoa kauli hiyo jana wakati Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akijibu maswali ya papo kwa papo kwa wabunge.

Mara baada ya Waziri Mkuu kumaliza kujibu swali la Mbunge wa Chemba, Juma Nkamia (CCM), Ndugai alisema nafasi ya kuuliza swali la kwanza katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu bungeni  imekuwa ikipotea kutokana na utoro wa kiongozi wa kambi hiyo.

“Waheshimiwa wabunge niwataarifu tu kwamba utaratibu wetu wa kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu swali la kwanza kabisa huwa linakuwa ‘reserved’ kwa kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni,” alisema Ndugai.

Alisema Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzania anaweza siku zote asiwepo bungeni, lakini Alhamisi ni muhimu awepo kutokana na Waziri Mkuu kuwepo na anatakiwa awe wa kwanza kuuliza swali.

“Huwa ni fursa pekee ambayo upinzani wanapata nafasi, kwa hiyo kiongozi wa upinzani anaweza asiwepo bungeni siku yoyote, lakini siku ya Alhamisi ambayo ni ya maswali kwa Waziri Mkuu anakuwepo,” alisema Ndugai.

Alisema hajapata taarafa zozote za Mbowe kutokuwepo bungeni, hivyo ni mtoro.

“Kwa hiyo hatujapata swali lile kwa kuwa kiongozi wa upinzani bungeni hayupo. Uwe wapi, uwe wapi kama Spika hana taarifa zako ni mtoro tu. Kwa hiyo, ni mtoro na ndiyo maana leo unaona kwamba hiyo fursa ambayo imewekwa kwenye kanuni haijaweza kutekelezwa.

“Na ndiyo maana mnaona kwamba nafasi inapotea potea sababu ya utoro,” alisema Spika Ndugai.

Katika hatua nyingine, Spika Ndugai jana alimkataza Mbunge wa Viti Maalumu, Devotha Minja (Chadema) kuuliza swali la papo kwa papo kwa Waziri Mkuu kwa madai kwamba alikuwa akisoma kwenye karatasi.

“Mheshimiwa Devotha kanuni zetu zinakataa mbunge kuandikiwa swali huko na kuja nalo hapa na kuanza kutusomea kwa jinsi hiyo, kwa kuwa swali hilo linaonekana rasmi sio la kwako bali umeandikiwa na watu huko, kwahiyo namwita Musa Bakari Mbarouk aulize swali lingine,” alisema Spika Ndugai.

Mara baada ya kauli hiyo ya Spika, Devotha alibaki ameduwaa asijue afanye nini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles